Ijumaa, 12 Juni 2015

Siku ya watoto hapa GCC - Wakatembelea Snake Park - Meserani

Tazama picha ujipatie maelezo mwenyewe

Ilifana sana
































Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2015/2016

HOTUBA YA MHESHIMIWA WAZIRI WA FEDHA, SAADA MKUYA SALUM (MB.), AKIWASILISHA BUNGENI MAPENDEKEZO YA SERIKALI KUHUSU MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI KWA MWAKA 2015/16 DODOMA, 11 JUNI, 2015 2

I. UTANGULIZI 1. Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja kwamba Bunge lako Tukufu lijadili na kupitisha Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka 2015/16. Pamoja na hotuba hii, tumeandaa vitabu vinne vya Bajeti vinavyoelezea takwimu mbalimbali za Bajeti. Kitabu cha Kwanza ni Makadirio ya Mapato; Kitabu cha Pili ni Makadirio ya Matumizi ya Kawaida kwa Wizara, Idara zinazojitegemea, Taasisi na Wakala za Serikali; Kitabu cha Tatu ni Makadirio ya Matumizi ya Kawaida kwa Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa; na Kitabu cha Nne ni Makadirio ya Matumizi ya Maendeleo kwa Wizara, Idara zinazojitegemea, Taasisi na Wakala za Serikali, Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa. Aidha, upo Muswada wa Sheria ya Fedha ya mwaka 2015 pamoja na Muswada wa Sheria ya Kuidhinisha Matumizi ya Serikali ya mwaka 2015 ambayo ni sehemu ya Bajeti hii. 3 2. Mheshimiwa Spika, naomba kuchukua fursa hii kutoa pole kwa ndugu, jamaa na marafiki na pia kwako wewe Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge wote kwa kuwapoteza marehemu Waheshimiwa Kapteni John Damiano Komba aliyekuwa Mbunge wa Mbinga Magharibi na Eugine Mwaiposa aliyekuwa Mbuge wa Ukonga ambao wametutangulia mbele ya haki. Tunawaombea kwa Mwenyezi Mungu awapumzishe kwa amani. 3. Mheshimiwa Spika, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia afya njema na kutuwezesha kushiriki mkutano wa kumi na moja wa Bunge la Kumi la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Namshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete kwa kuendelea kuniamini kutumikia Taifa katika nafasi ya Waziri wa Fedha. Aidha, nampongeza Mheshimiwa Rais kwa uongozi wake thabiti na wenye mafanikio makubwa katika awamu hii ya nne. Vilevile, ninamshukuru Makamu wa Rais Mheshimiwa Dkt. Mohamed Gharib Bilal pamoja na Waziri Mkuu Mheshimiwa 4 Mizengo Kayanza Peter Pinda (Mb) kwa maelekezo mazuri kwangu katika kazi zangu za kila siku. Napenda pia kutumia fursa hii kukushukuru na kukupongeza wewe Mheshimiwa Spika, Naibu Spika na Wenyeviti wa vikao vya Bunge kwa kuongoza vizuri majadiliano kwa muda wote wa uhai wa Bunge hili. 4. Mheshimiwa Spika, napenda kutoa shukrani kwa Viongozi na Watendaji wa Wizara, Idara za Serikali zinazojitegemea, Wakala na Taasisi za Serikali, Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa na wadau mbalimbali kwa kushiriki kwa namna moja au nyingine kufanikisha matayarisho ya Bajeti ya mwaka 2015/16. Natoa pia pongezi zangu za dhati kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti chini ya uongozi makini wa Mheshimiwa Dkt. Festus Limbu (Mb) na Mheshimiwa Kidawa Salehe (Mb), pamoja na kamati za kisekta kwa ushauri na mapendekezo mbalimbali ambayo yamezingatiwa katika Bajeti hii. Vilevile, ninapenda kumshukuru kipekee Mheshimiwa Dkt. Mary Nagu (Mb), Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Mahusiano na Uratibu kwa kunipa ushirikiano mzuri katika kuandaa Bajeti. 5 5. Mheshimiwa Spika, napenda pia kutumia fursa hii kuwashukuru Naibu Mawaziri, Mheshimiwa Adam Kighoma Ali Malima (Mb.) na Mheshimiwa Mwigulu Lameck Madelu Nchemba (Mb.) kwa ushirikiano wao. Namshukuru Waziri wa Fedha wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Mheshimiwa Omari Yusuf Mzee kwa ushirikiano wake aliotupa wakati wa matayarisho ya bajeti hii. Aidha, napenda kutoa shukrani za dhati na za kipekee kwa Katibu Mkuu Dkt. Servacius B. Likwelile kwa kuisimiamia vizuri kazi ya kuandaa Bajeti hii akisaidiwa na Manaibu wake Profesa Adolf F. Mkenda, Bibi Dorothy S. Mwanyika na Dkt. Hamisi H. Mwinyimvua. Vilevile, napenda kuwashukuru Katibu Mtendaji wa Tume ya Mipango, Dr. Phillip Mpango, Gavana wa Benki Kuu, Profesa Benno Ndulu, Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania Bw. Rished Bade, Msajili wa Hazina Bwana Laurence Mafuru, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Ofisi ya Mpigachapa Mkuu wa Serikali kwa kufanikisha maandalizi ya Bajeti hii. Kwa namna ya pekee napenda kuwashukuru Kamishna wa Bajeti, Bw. John Cheyo, Kamishna wa Sera, Bw. Bedason Shallanda na Kamishna 6 wa Fedha za Nje, Bw. Ngosha Magonya kwa kazi nzuri ya kiufundi waliyofanya katika kuandaa Bajeti hii, kazi ambayo wameifanya kwa weledi na juhudi kubwa. Nawashukuru Wakuu wote wa Idara na Vitengo, Taasisi na Wakala za Serikali zilizo chini ya Wizara ya Fedha pamoja na wafanyakazi wote wa Wizara ya Fedha kwa kazi nzuri waliofanya katika kuandaa Bajeti hii. 6. Mheshimiwa Spika, Bajeti ya mwaka 2015/16 ni ya kipekee kwa sababu kadhaa. Kwanza ni Bajeti ya mwaka wa Uchaguzi Mkuu ambapo Serikali ya Awamu ya Nne inamaliza muda wake na Serikali mpya ya Awamu ya Tano inatarajiwa kuingia madarakani. Kwa mantiki hiyo, hii ni Bajeti ya mwisho katika utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2010. Pili, utekelezaji wa MKUKUTA II ulipangwa kufikia tamati Juni, 2015. Hata hivyo, Serikali imeamua kuongeza muda wa kutekeleza MKUKUTA II hadi Juni 2016, ili utekelezaji wake ukamilike sawia na kumalizika kwa utekelezaji wa Mpango wa Kwanza wa Maendeleo wa Miaka Mitano. 7 7. Mheshimiwa Spika, lengo la kufanya hivyo ni kutumia fursa hii kufanya tathmini ya kina ya MKUKUTA II na Mpango wa Maendeleo, na kutumia matokeo ya tathmini hizo katika kupanga mpango wa pili wa miaka mitano utakaoanza Juni 2016 hadi Juni 2021. Ni azma ya Serikali kuhakikisha kuwa mpango mpya wa maendeleo wa miaka mitano utakaozinduliwa Juni 2016 utaunganisha mambo yote yanayohusu kukuza uchumi hasa katika nyanja ya viwanda pamoja na kupunguza umasikini, mambo ambayo yamekuwa yakishughulikiwa kupitia MKUKUTA. 8. Mheshimiwa Spika, Bajeti hii ina vipaumbele vichache vifuatavyo. Kwanza, kugharamia shughuli za Uchaguzi Mkuu ikiwa ni pamoja na gharama zote za shughuli za Bunge lijalo, Mabaraza ya Madiwani na shughuli za Serikali awamu ya nne na kuanza kazi kwa bunge lĂ­jalo. Pili, kuweka msukumo katika kukamilisha miradi inayoendelea; na tatu, kuweka msukumo maalum kwenye miradi ya umeme na maji vijijini na kuimarisha rasilimali watu. Ili kutekeleza hayo, msisitizo mkubwa utawekwa kwenye kukusanya mapato ya ndani. 8 Mtazamo Mpya wa Mapato ya Ndani 9. Mheshimiwa Spika, napenda kuzungumzia mwelekeo wa mageuzi kwenye suala la misamaha ya kodi. Jambo la kwanza linahusu mwelekeo wa mageuzi ya kodi. Kwa muda sasa Serikali imekuwa ikipunguza misamaha ya kodi inayotolewa kwa ridhaa ya Waziri wa Fedha kwa mujibu wa sheria. Badala ya kutoa misamaha kwa ridhaa, Serikali imechukua mwelekeo wa kupunguza au kuondoa kodi kwenye bidhaa zenye umuhimu wa kipekee, ili yeyote anayenunua bidhaa hizo awe na nafuu ya kodi moja kwa moja, bila kutegemea ridhaa ya waziri. 10. Mheshimiwa Spika, Sheria mpya ya Kodi ya Ongezeko la Thamani ambayo itaanza kutumika tarehe mosi Julai, 2015 Serikali imeondoa kodi kwa bidhaa muhimu kama vile pembejeo, zana za kilimo, zana za uvuvi, vifaa tiba pamoja na bidhaa zote za mitaji. Hivyo, mwananchi atakaponunua bidhaa hizo hatatozwa kodi. Huu ndio mwelekeo wa mageuzi tunayoyafanya katika kupunguza 9 misamaha ya kodi inayotolewa kwa ridhaa (discretionary). Kauli mbiu ya mageuzi haya ni “punguza ridhaa ongeza bidhaa”, yaani kupunguza misamaha ya kodi inayotolewa kwa ridhaa na badala yake kupunguza kodi kwenye bidhaa zenye umuhimu maalum kwa wananchi na uchumi itakayotolewa moja kwa moja kwenye Sheria. Lengo kuu ni kuhakikisha usawa, haki na ufanisi katika kodi na kupunguza mianya ya upendeleo na hata rushwa katika utoaji wa misamaha ya kodi kwa ridhaa. 11. Mheshimiwa Spika, pamoja na mwelekeo huu wa kupunguza misamaha ya kodi kwa ridhaa, bado Serikali inatambua umuhimu wa kutoa misamaha ya kodi kimkakati kwa kipindi maalumu ili kuvutia wawekezaji wakubwa wanaowekeza fedha nyingi na kuzalisha ajira nyingi kwa Watanzania. Hata hivyo, ni muhimu misamaha hii itolewe kwa uwazi na kuwe na ufuatiliaji, tathmini na uwajibikaji wa kutosha kama Bunge lako Tukufu linavyoelekeza mara zote. Serikali imeweka mapendekezo kwenye Muswada wa Fedha wa mwaka 2015/16 wa namna ya kutambua wawekezaji mahsusi wa kimkakati (special strategic investors) 10 ambao wataweza kupewa misamaha mahsusi ya kodi itakayopendekezwa na Waziri wa Fedha ili kupata idhini ya Bunge lako tukufu. 12. Mheshimiwa Spika, mwekezaji mahsusi wa kimkakati anapaswa kuwa na sifa zifuatazo: awe na mtaji usiopungua dola za Marekani milioni mia tatu na mtaji wa kifedha upitie kwenye taasisi za fedha za humu nchini ikiwa pamoja na huduma za bima; na uwekezaji huo ulete ajira kwa Watanzania zisizopungua watu elfu moja na mia tano. Wawekezaji hao wanatakiwa kuzingatia Sera ya Uwezeshaji ya mwaka 2004 na kutumia huduma na bidhaa zinazozalishwa hapa nchini. 13. Mheshimiwa Spika, tunafanya taratibu hizi ili kuhakikisha kuwa sera zetu za kodi zinazingatia usawa na haki na pia kuchochea ukuaji wa uchumi wetu. Kwa kuzingatia mwelekeo huu, Wizara ya Fedha inaendelea kutangaza misamaha yote ya kodi tunayoitoa ili kila mwananchi ajue ni nani ananufaika na misamaha hii na sababu ya kuitoa misamaha hiyo. Taarifa ya 11 misamaha ya kodi inapatikana katika tovuti ya Wizara ya Fedha - www.mof.go.tz Marekebisho ya Mfumo wa Bajeti 14. Mheshimiwa Spika, kama itakavyokumbukwa, Aprili 2015 niliwasilisha Mfumo wa Bajeti mbele ya waheshimiwa wabunge wote walipokaa kama kamati. Katika Mfumo huo, niliwasilisha mapendekezo ya mapato na matumizi yenye jumla ya shilingi bilioni 22,769.1 ambapo mapato ya kodi yalikuwa shilingi bilioni 13,361.2 na mapato yasiyo ya kodi shilingi bilioni 1,009.2 Hata hivyo, baada ya majadiliano ya kina na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti, tulikubali tahadhari ya Kamati kwamba, maoteo ya mapato ya kodi yaliyotumika kwenye mfumo huo hayaendani na mwenendo wa makusanyo katika miaka ya karibuni. Kamati ya Bajeti ilipendekeza Serikali ipunguze ukubwa wa bajeti na kushusha maoteo ya mapato yatokanayo na kodi. Kamati ya Bajeti ilishauri kwamba, pamoja na matumaini ya Serikali kwamba itaweza kufikia lengo la makusanyo lililowekwa, 12 itakuwa busara kupunguza matumizi hadi hapo lengo la mapato la awali litakapofikiwa, ambapo Serikali itabidi kurudi bungeni kuomba kibali cha matumizi ya ziada (supplementary budget). 15. Mheshimiwa Spika, kama nilivyoeleza, tulikubaliana na ushauri wa Kamati ya Kudumu ya Bajeti kwa sababu bado kuna fursa ya kurudi bungeni katikati ya mwaka wa fedha endapo makusanyo yaliyokusudiwa yatafikiwa na kuomba kibali cha kurudisha fedha ambazo zimepunguzwa kwenye mafungu katika Mfumo wa Bajeti unaopendekezwa sasa. Kutokana na makato hayo, tunawasilisha Jedwali lenye marekebisho ya mgao wa fedha kwenye mafungu kulingana na mfumo unaopendekezwa sasa. Pamoja na kupunguza fedha kwenye mafungu, tumeongeza nakisi ya bajeti kufikia asilimia 4.2 ya Pato la Taifa ili kuiwezesha Serikali kulipia malimbikizo yote yaliyohakikiwa ya madai ya makandarasi, wazabuni, watumishi wa Serikali pamoja na sehemu ya deni la PSPF kwenye mwaka wa fedha 2015/16. Kutokana na maelezo hayo, Mfumo wa Mapato na Matumizi ninaouwasilisha katika hotuba hii ni wenye jumla ya mapato ya shilingi bilioni 22,495.5, 13 ambapo mapato ya kodi ni shilingi bilioni 12,363 na mapato yasiyo ya kodi shilingi bilioni 1,112.7. Mfumo mzima wa Bajeti unaonekana katika Jedwali lenye Sura ya Bajeti ya mwaka 2015/16. Marekebisho hayo yanabadilisha viwango vilivyowasilishwa hapo awali kwenye vitabu vya matumizi namba II III na IV. Bajeti ya mwaka 2015/16 ya shilingi bilioni 22,495.5 imeongezeka kwa shilingi bilioni 2,642.2 ikilinganishwa na bajeti ya shilingi bilioni 19,853.3 ya mwaka 2014/15. Dhamira ya Kuongeza Makusanyo ya Mapato 16. Mheshimiwa Spika, pamoja na kurekebisha mfumo wa Bajeti kwa tahadhari, bado dhamira ya Serikali ni kuhakikisha kwamba katika mwaka ujao wa fedha, makusanyo ya kodi yanaongezeka. Kwa sasa makusanyo ya mapato ya kodi ni takribani asilimia kumi na mbili ya Pato la Taifa, kiwango ambacho ni cha chini ikilinganishwa na nchi nyingi jirani. Nina uhakika kuwa tunao uwezo wa kuongeza mapato ya kodi. Tutafanya hivyo kwa kuwa na mikataba ya utendaji na Mamlaka ya Mapato Tanzania 14 (TRA), yaani ‘performance contracts’, kuanzia ngazi ya juu mpaka wasimamizi wa chini ili kuhakikisha tunafikia malengo ya ukusanyaji. Utendaji wa TRA na hasa wa watendaji wake wenye mamlaka ya usimamizi utapimwa kwa namna wanavyofikia malengo yao ya ukusanyaji wa mapato ya kodi. Tutaongeza pia jitihada za kuziba mianya ya kukwepa kodi. Aidha, napenda kuchukua fursa hii kumshukuru sana Mheshimiwa Omar Yusuf Mzee, Waziri wa Fedha wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, kwa kuunga mkono jitihada za TRA za kutumia mfumo wa Tanzania Customs Integrated System yaani TANCIS, pamoja na mfumo mmoja wa ukadiriaji wa thamani za bidhaa, yaani Centralized Price-Based Valuation System, ili mifumo hii muhimu itumike kote katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Vilevile, matumizi ya mifumo hii yatapunguza sana ukwepaji wa kodi, na zaidi ya hapo, itaondoa kabisa ulazima wa TRA kukadiria thamani ya bidhaa zinazoingia Tanzania Bara kutokea Zanzibar. Hii ni hatua kubwa sana katika kumaliza kero ya Muungano kwa waingizaji wa bidhaa kati ya Zanzibar na Tanzania Bara, na TRA ni lazima sasa iongeze kasi kusambaza mifumo hii. 15 17. Mheshimiwa Spika, hatua nyingine tutakazozichukua ni kupiga marufuku Serikali kutumia wazabuni ambao hawalipi kodi kikamilifu. Serikali, Wakala wa Serikali na Mamlaka za Serikali za Mitaa haitafanya biashara na mzabuni yeyote ambaye hatumii mashine za EFD. 18. Mheshimiwa Spika, ukusanyaji wa mapato yasiyo ya kodi pia utaimarishwa kwa kuchukua hatua mbalimbali. Kwanza, ni lazima mfumo wa kieletroniki utumike katika utoaji wa risiti kwa tozo, faini, ada na malipo mengine yote ya Serikali kuu, Mamlaka za Serikali za Mitaa na Wakala wote wa Serikali. Narudia. Ni lazima sasa mfumo wa kieletroniki utumike katika utoaji wa risiti kwa tozo, faini, ada na malipo mengine yote ya Serikali kuu, mamlaka za serikali za mitaa na wakala wote wa Serikali. Hii itahusisha pia malipo ya faini mahakamani, faini za usalama barabarani, viingilio kwenye mbuga za wanyama, vibali vya kuvuna maliasili, na kadhalika. Maafisa masuuli wote wanapaswa kusimamia utekelezaji wa agizo hili. Pili, Wizara, Wakala na Mamlaka za 16 Serikali za Mitaa zitapunguziwa migao ya kila mwezi kwa kiwango watakachokua wameshindwa kukusanya maduhuli kwa mwezi husika. Tatu, Wizara ya Fedha itaangalia uwezekano wa kuingia mikataba ya utekelezaji (performance contracts) ya ukusanyaji wa mapato na mamlaka za serikali za mitaa ili kuhimiza ukusanyaji stahiki. Nne, tunaongeza kasi ya kufanya tathmini ya majengo mijini ili kuhakikisha tozo stahiki zinalipwa. Tano, Serikali itapitia upya utaratibu wa kutumia mawakala katika ukusanyaji wa mapato ya mamlaka za serikali za mitaa. Sita, mashirika ya umma na wakala za serikali zitasimamiwa kwa karibu zaidi na Msajili wa Hazina ili kuhakikisha Serikali inapata gawio stahiki, ubadhirifu unaondolewa na mapato ya ziada yanachangia Mfuko Mkuu wa Serikali. Moja ya hatua muhimu katika hili ni kupitia upya viwango vya posho za safari katika taasisi na mashirika ya umma. 19. Mheshimiwa Spika, jitihada hizi za kuongeza mapato zitatusaidia pia kupunguza utegemezi wa Bajeti ya Serikali kwa fedha za wahisani. Kwa hakika, Serikali imeendelea kuchukua hatua za makusudi zenye lengo la kupunguza utegemezi wa bajeti 17 ambapo kiwango cha utegemezi kimepungua kutoka asilimia 24 mwaka 2004/05, asilimia 17 mwaka 2010/11, na kufikia asilimia 6.4 mwaka 2015/16. Hii ni hatua kubwa na ya kujivunia. Ni matumaini yangu kuwa Waheshimiwa Wabunge na Wananchi wote wataunga mkono dhamira hii. Kuimarisha Usimamizi wa Matumizi 20. Mheshimiwa Spika, sambamba na jitihada za kuongeza makusanyo, Serikali itasimamia kwa umakini matumizi ya fedha za umma. Katika kutekeleza azma hiyo, Serikali itakamilisha kanuni za Sheria ya Bajeti ya mwaka 2014 na kuitekeleza. Aidha, madai ya wazabuni yasiyoambatishwa na LPO iliyotolewa kwenye mtandao wa malipo wa IFMS hayatatambuliwa kama madai halali. Vilevile, Serikali itaendelea kusimamia Sheria ya Ununuzi wa Umma ili kuepuka kutoa zabuni ambazo hazikutengewa fedha na hivyo kuepuka malimbikizo ya madai. Kadhalika, utoaji wa fedha kwa mafungu utaendelea kuzingatia mapato na uwasilishwaji wa taarifa za matumizi. Malipo ya madeni ya Serikali yatafanyika 18 baada ya kuhakikiwa na Mkaguzi Mkuu wa Ndani wa Serikali. Hatua hizi zimekusudia kuondoa tatizo la malimbikizo ya madai. Madeni ya Mifuko ya Hifadhi ya Jamii na Wazabuni 21. Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua kuwepo kwa madeni inayodaiwa na Mifuko ya Hifadhi ya Jamii. Madeni hayo yametokana na mifuko hiyo kutekeleza miradi mbalimbali ya Serikali pamoja na yale ya Mfuko wa PSPF yaliyotokana na ulipaji wa mafao kwa wastaafu wenye utumishi wa kabla ya tarehe 1 Julai, 1999, ambao hawakuchangia katika Mfuko. Hivyo basi, katika mwaka wa fedha 2015/16, Serikali imedhamiria kulipa madeni hayo ya Mifuko ya Hifadhi ya Jamii kwa utaratibu wa kutoa hatifungani maalum zisizo taslimu (Non Cash Special Bond) na kuendelea kutenga kiasi cha fedha kwenye bajeti ya Serikali ili kulipia deni kutokana na wastaafu wanaolipwa mafao bila kuchangia kabla ya mwaka 1999. Hatifungani zitakazotolewa zitakuwa na muda wa kuiva (maturity) tofauti tofauti kwa kuzingatia mpangilio wa kuiva kwa dhamana nyingine za Serikali 19 (maturity profile). Utaratibu huu utaiwezesha Serikali kutambua madeni hayo kwenye Deni la Taifa na pia utaiwezesha Mifuko ya Hifadhi ya Jamii kupata kiasi cha fedha kutokana na riba itakayokuwa inalipwa na Serikali kila mwaka, pamoja na uwezo wa kuuza hatifungani hizo kwenye Soko la Pili (Secondary Market), na hivyo kuimarisha hali ya kifedha ya Mifuko. 22. Mheshimiwa Spika, miaka ya hivi karibuni kumekuwa na malimbikizo ya madai mbalimbali yakiwemo madai ya makandarasi, wazabuni na watumishi. Serikali imedhamiria kulishughulikia tatizo hili kwa kuimarisha mifumo ya usimamizi na udhibiti wa matumizi ya fedha za umma na kulipa madai yaliyohakikiwa. Aidha, hadi kufikia Aprili 2015, jumla ya madai ya shilingi bilioni 692.2 yalilipwa. Vilevile, Serikali inategemea kulipa shilingi bilioni 200 zaidi kabla ya mwisho wa Juni 2015, ambapo kati ya hizo, shilingi bilioni 57.7 zimetolewa. Madai yaliyobaki ambayo yamehakikiwa yametengewa fedha katika Bajeti ya mwaka 2015/16. 20 Maslahi ya Watumishi wa Umma 23. Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuboresha maslahi ya watumishi wa umma ikiwa ni pamoja na kuongeza mshahara wa kima cha chini kutoka shilingi 65,000 mwaka 2005 hadi kufikia 265,000 mwaka 2014/15 ikiwa ni ongezeko la asilimia 307.7 Aidha, Serikali imeendelea kufanya marekebisho ya mfumo wa kodi ya mishahara (PAYE) kwa kupunguza kiwango cha kodi cha chini kutoka asilimia 18.5 mwaka 2006/07 hadi asilimia 11 mwaka 2015/16 ikiwa ni punguzo la asilimia 35. Pensheni kwa Wastaafu 24. Serikali inatambua umuhimu wa wastaafu ambao walitoa mchango mkubwa kwa taifa hili. Kwa kuzingatia hilo, katika mwaka 2015/16, Serikali itaongeza kima cha chini cha pensheni kwa wastaafu wa Serikali kwa mwezi kutoka shilingi 50,000 hadi shilingi 85,000 sawa na ongezeko la asilimia 70. 21 Mafao kwa Wazee 25. Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kutambua mchango wa wazee wetu katika kujenga Taifa hili, imedhamiria kuwalipa mafao ya kila mwezi. Aidha, kwa sasa Serikali imeanza zoezi la kuandaa mfumo na utaratibu wa kuwatambua wazee wote nchini ili kupata idadi kamili ya wazee na kuhakikisha kwamba mafao yanawafikia walengwa kwa wakati. Kwa kuzingatia hilo, katika mwaka 2015/16, Serikali inatarajia kuanza maandalizi ya kuwezesha kufanya malipo hayo. Maandalizi hayo ni pamoja na kutunga Sheria stahiki, kuwatambua kupitia Serikali za Mitaa kwa kutumia mfumo shirikishi jamii na kuweka utaratibu wa kuwalipa. 26. Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo ya awali, naomba sasa kutoa taarifa kuhusu mapitio ya utekelezaji wa bajeti ya mwaka 2014/15 na makadirio ya mapato na matumizi kwa kipindi cha mwaka 2015/16. 22

II. MAPITIO YA UTEKELEZAJI WA SERA ZA BAJETI YA MWAKA 2014/15 27. Mheshimiwa Spika, Sera za bajeti za mwaka 2014/15, zilijikita katika kukuza uchumi, kudhibiti kasi ya upandaji bei, kupunguza misamaha ya kodi pamoja na kuongeza mapato. Katika kipindi hicho, Serikali ilipanga kupata mapato ya jumla ya shilingi bilioni 19,853.3 kutoka kwenye vyanzo vya ndani na nje. Aidha, ilipanga kutumia kiasi cha shilingi bilioni 13,408.2 kwa ajili ya matumizi ya kawaida na shilingi bilioni 6,445.1 kwa ajili ya matumizi ya maendeleo kutokana na mapato yaliyotarajiwa. Mwenendo wa ukusanyaji wa mapato ya ndani 28. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2014/15, sera za mapato zililenga kukusanya mapato ya kodi na yasiyo ya kodi ya kiasi cha shilingi bilioni 12,178. Aidha, makadirio ya mapato ya mamlaka za Serikali za Mitaa yalikuwa shilingi bilioni 458.5. Katika kipindi cha Julai 2014 hadi Aprili 2015, jumla ya makusanyo ya kodi na yasiyo ya kodi yalikuwa shilingi bilioni 8,640.9 sawa na 23 asilimia 86 ya makadirio ya shilingi bilioni 9,991. Mapato ya mamlaka za Serikali za Mitaa yalikuwa shilingi bilioni 284 sawa na asilimia 62 ya makadirio ya shilingi bilioni 458.5 kwa mwaka. 29. Mheshimiwa Spika, hadi Aprili 2015, mapato ya kodi yalifikia shilingi bilioni 8,106.5 sawa na asilimia 72 ya makadirio ya mwaka ya shilingi bilioni 11,318.2. Inakadiriwa hadi tarehe 30 Juni, 2015 mapato ya kodi yatafikia asilimia 91 ya lengo la mwaka. Kutofikia lengo la makusanyo ya kodi kulitokana na: kushuka kwa makusanyo yatokanayo na shughuli za utafiti na uchimbaji wa gesi, mafuta na madini hususan kodi ya zuio; makusanyo hafifu kutoka kwenye ushuru wa bidhaa za vinywaji baridi, sigara, bia na tozo za huduma za kibenki; kuendelea kuwepo kwa mwitikio hafifu kutoka kwa wafanyabiashara kwenye utumiaji wa mashine za kielektroniki (EFD); pamoja na kupungua kwa ukuaji wa uagizaji wa bidhaa zisizo za kimtaji. 30. Mheshimiwa Spika, kwa upande wa mapato yasiyo ya kodi, hadi Aprili, 2015 yalifikia shillingi billioni 534.4 ikiwa ni 24 asilimia 62 ya lengo la kukusanya shillingi billioni 859.9 kwa mwaka. Inakadiriwa hadi tarehe 30 Juni, 2015 mapato yasiyo ya kodi yatafikia asilimia 74 ya lengo la mwaka. 31. Mheshimiwa Spika, kwa upande wa mapato ya mamlaka za Serikali za Mitaa shilingi bilioni 296.7 zilikusanywa hadi Aprili 2015, ikiwa ni asilimia 65 ya makadirio ya mwaka ya shillingi billioni 458.5. Inakadiriwa hadi tarehe 30 Juni, 2015 mapato ya mamlaka za Serikali za Mitaa yatafikia asilimia 78 ya lengo la mwaka. Sababu ya kutofikiwa kwa malengo hayo ni pamoja na zoezi la uthamini wa majengo kutokamilika na hivyo kuathiri ukusanyaji wa kodi ya majengo na kutotumika kwa mfumo wa kielektroniki katika ukusanyaji wa mapato. 32. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha kuanzia Julai, 2014 hadi kufikia Aprili, 2015 misamaha ya kodi ilifikia kiasi cha shilingi bilioni 1,301.2, sawa na asilimia 1.4 ya Pato la Taifa. Hadi kufikia mwisho wa mwezi Juni, 2015 misamaha ya kodi inatarajiwa kufikia jumla ya shilingi bilioni 1,419.5 sawa na asilimia 1.5 ya Pato la 25 Taifa, ikilinganishwa na misamaha ya kodi ya sawa na asilimia 2.0 ya Pato la Taifa iliyotolewa katika kipindi kama hiki kwa mwaka 2013/14. Misaada na Mikopo ya Nje yenye Masharti Nafuu 33. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2014/15, Serikali ilitarajia kupata mikopo ya masharti nafuu na misaada kutoka kwa Washirika wa Maendeleo ya takribani shilingi bilioni 2,941.5. Hadi kufikia Aprili, 2015, misaada na mikopo ya kibajeti iliyopokelewa ilifikia shilingi bilioni 408 sawa na asilimia 44 ya makadirio ya mwaka ya shilingi bilioni 922.2. Aidha, fedha zilizopokelewa kwenye mifuko ya kisekta ni shilingi bilioni 289.5 sawa na asilimia 106 ya makadirio ya shilingi bilioni 274.1 kwa mwaka. Kwa upande wa mikopo na misaada ya miradi ya maendeleo, shilingi bilioni 1,117 zilipokelewa ambazo ni sawa na asilimia 64 ya makadirio ya mwaka ya shilingi bilioni 1,745.3. Inakadiriwa kuwa hadi tarehe 30 Juni, 2015 misaada na mikopo ya nje yenye masharti nafuu itafikia asilimia 70 ya lengo la mwaka. Kutofikia 26 lengo kunatokana na baadhi ya Washirika wa Maendeleo wanaochangia GBS kutotimiza ahadi zao pamoja na kasi ndogo ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo. Mikopo ya Kibiashara ya Ndani 34. Mheshimiwa Spika, mwaka 2014/15, Serikali ilipanga kukopa kiasi cha shilingi bilioni 2,955.2 kutoka kwenye soko la ndani kwa ajili ya kugharimia miradi ya maendeleo na kulipia amana na hatifungani za Serikali zilizoiva (roll over). Kati ya kiasi hicho, shilingi bilioni 686.4 ilikuwa ni mikopo mipya kwa ajili ya kugharamia miradi ya maendeleo na shilingi bilioni 2,265.7 ilikuwa ni mikopo kwa ajili ya kulipia dhamana za Serikali zilizoiva. Hadi Aprili, 2015, shilingi bilioni 1,767.9 zilikopwa kwa ajili ya kulipia dhamana na hatifungani za Serikali zilizoiva. Mikopo ya Kibiashara kutoka Nje 35. Mheshimiwa Spika, mwaka 2014/15, Serikali ilipanga kukopa dola za Marekani milioni 800 sawa na shilingi bilioni 27 1,320.01 kutoka kwenye vyanzo vya nje vya kibiashara ili kugharimia miradi ya maendeleo. Hadi Aprili 2015, Serikali imekopa dola milioni 300 (sawa na shilingi bilioni 5142 ) kutoka Benki ya Maendeleo ya China (CDB), kiasi hiki ni asilimia 39 ya kiwango kinachopaswa kukopwa kwa mwaka. Kutokupatikana kwa mikopo kwa kiwango kilichopangwa kwa wakati kunatokana na masharti ya mikopo yanayo badilika mara kwa mara ya soko la fedha duniani na kutokana na mchakato mrefu wa majadiliano. Hata hivyo, taratibu za kukamilisha upatikanaji wa fedha zilizobakia zinaendelea. Sera za Matumizi 36. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2014/15, sera za matumizi zilijielekeza katika: kuwianisha matumizi na mapato yanayotarajiwa; kuimarisha zaidi usimamizi na udhibiti wa matumizi ya fedha za umma, ikiwa ni pamoja na kuandaa Sheria 1 Kiwango cha kubadilisha dola kilikuwa shilingi 1,650 kwa wakati huo 2 Kiwango cha kubadilisha dola kilikuwa shilingi 1,713.33, kwa wakati huo 28 ya Bajeti; kuhimiza matumizi ya mashine za kielektroniki katika ununuzi unaofanywa na Serikali na Taasisi za umma; Wakala na Mamlaka za Serikali za Mitaa kuwasilisha bajeti zao na kuidhinishwa na Mlipaji Mkuu wa Serikali; kuendelea kuhakiki madai kabla ya kulipwa; na kuzingatia ununuzi wa pamoja kutoka kwa wazalishaji badala ya wakala. 37. Mheshimiwa Spika, sera hizi za matumizi zimetekelezwa kwa mafanikio ya kuridhisha, ikiwa ni pamoja na kutungwa kwa Sheria ya Bajeti ambapo utekelezaji wake utaanza tarehe 1 Julai 2015; kuanza kutumika kwa utaratibu wa ununuzi wa pamoja kwa magari ya Serikali ambapo hadi Aprili 2015, shilingi bilioni 2 zimeokolewa kutokana na ununuzi wa magari 50; kuanza uchambuzi na uidhinishwaji wa bajeti za taasisi na wakala; uhakiki wa madai kabla ya kulipwa unaendelea na matumizi ya EFDs kwa Serikali na taasisi zake umeanza kutumika. 29 Mwenendo wa Matumizi 38. Mheshimiwa Spika, hadi kufikia Aprili, 2015, Serikali imetoa mgao wa fedha za matumizi wenye jumla ya shilingi bilioni 14,121.4 kwenye mafungu mbalimbali kwa ajili ya utekelezaji wa Bajeti. Kati ya kiasi kilichotolewa, shilingi bilioni 11,543.3 zilikuwa ni matumizi ya kawaida ikijumuisha mishahara ya watumishi wa Serikali na Taasisi yenye jumla ya shilingi bilioni 4,349.1, Mfuko Mkuu wa Serikali (CFS) shilingi bilioni 4,467.9, shilingi bilioni 2,726.3 za matumizi mengineyo; na shilingi bilioni 2,578.1 kwa ajili ya matumizi ya maendeleo. Matumizi ya Kawaida 39. Mheshimiwa Spika, hadi kufikia Aprili 2015, malipo ya riba ya deni la ndani na nje yalifikia shilingi bilioni 921.2. Kati ya kiasi hicho, malipo ya riba ya deni la ndani ni shilingi bilioni 629.7 na riba ya deni la nje ni shilingi bilioni 291.6. Aidha, malipo ya mikopo yalifikia shilingi bilioni 1,878. Kati ya malipo hayo, shilingi 30 bilioni 110 ni malipo ya mikopo ya nje na shilingi bilioni 1,767.9 ni malipo ya mikopo ya ndani. Matumizi mengine ya Mfuko Mkuu (CFS Others) yalikuwa shilingi bilioni 929.9. 40. Mheshimiwa Spika, malipo ya mishahara ya watumishi wa Serikali yalikuwa shilingi bilioni 4,349.1. Kati ya fedha hizo, shilingi bilioni 1,822.9 zililipwa kwa watumishi wa Serikali Kuu, shilingi bilioni 106.3 zilitolewa kwa ajili ya watumishi wa Sekretarieti za Mikoa na shilingi bilioni 2,419.8 kwa ajili ya mishahara ya watumishi katika mamlaka za Serikali za Mitaa. Aidha, Serikali ililipa mishahara ya Taasisi na Mashirika ya Umma jumla ya shilingi bilioni 530.0. Vilevile, shilingi bilioni 2,726.3 zimetolewa kama matumizi mengineyo, ambapo sehemu kubwa ya matumizi haya imegharamia maandalizi ya Uchaguzi Mkuu, ununuzi wa Chakula cha Hifadhi ya Taifa, ruzuku ya pembejeo za kilimo, mitihani ya shule za msingi na sekondari, Bunge la Katiba pamoja na ulipaji wa madeni madai mbalimbali. Matumizi ya Maendeleo 31 41. Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kutekeleza bajeti ya maendeleo kwa mwaka 2014/15 kwa kuwianisha mapato na matumizi. Aidha, vigezo vingine vinavyotumika ni pamoja na: Mapendekezo ya Tume ya Mipango yanayozingatia utaratibu wa Tekeleza kwa Matokeo Makubwa Sasa; uwasilishaji wa taarifa za utekelezaji; uwasilishaji wa hati za madai kwa miradi ya ujenzi; uwasilishaji wa taarifa za matumizi ya fedha kwa kila mwezi kwa fedha zilizokwishapokelewa, pamoja na uwasilishaji wa mpango kazi na mtiririko wa mahitaji ya fedha. 42. Mheshimiwa Spika, hadi kufikia Aprili, 2015, shilingi bilioni 2,578.1 zilitolewa kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo. Kati ya kiasi hicho, shilingi bilioni 1,998.9 ni fedha za ndani na shilingi bilioni 579.2 ni fedha za nje. Aidha, shilingi bilioni 649.5 zimeelekezwa kwenye mafungu yanayotekeleza miradi ya Tekeleza kwa Matokeo Makubwa Sasa, ambapo shilingi bilioni 544.8 ni fedha za ndani na shilingi bilioni 104.7 ni fedha za nje. Fedha hizo zilitolewa katika sekta zifuatazo: Nishati shilingi bilioni 32 302.5; Elimu shilingi bilioni 129.1; Uchukuzi shilingi bilioni 105.3; Maji shilingi bilioni 81; Kilimo shilingi bilioni 30; na ukusanyaji mapato shilingi bilioni 1.5. Usimamizi na Udhibiti wa Matumizi ya Fedha za Umma 43. Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kusimamia uwazi na uwajibikaji katika matumizi ya fedha za umma na kuendelea kuandaa taarifa za hesabu zinazokidhi mahitaji ya Viwango vya Kimataifa vya Uhasibu Katika Sekta ya Umma- IPSAS Accrual Basis. Katika mwaka 2013/14, kwa mara ya kwanza, Serikali iliandaa na kuwasilisha kwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, hesabu za majumuisho zilizounganisha hesabu za Serikali Kuu, Mamlaka za Serikali za Mitaa, Mashirika na Taasisi mbalimbali kwa kuzingatia viwango hivyo. 44. Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuimarisha udhibiti wa matumizi ya fedha za umma kwa kupanua mtandao wa malipo kupitia benki, yaani TISS, ambapo mikoa yote ya Tanzania Bara inalipa kwa kutumia utaratibu huu. Aidha, kuanzia 33 Julai 2015, Serikali itaendelea na zoezi la kupanua mtandao wa TISS ili kuzifikia mamlaka zote za Serikali za Mitaa nchini kwa ajili ya kuboresha na kudhibiti matumizi ya fedha za umma. Vilevile, wastaafu waliohakikiwa na kuorodheshwa kwenye daftari la wastaafu wanapata malipo yao ya pensheni moja kwa moja kwenye akaunti zao za benki kwa kutumia mfumo huu. Utekelezaji wa Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umaskini Tanzania (MKUKUTA-II) 45. Mheshimiwa Spika, katika kupima matokeo ya utekelezaji wa MKUKUTA-II, Serikali iliendelea kufanya ufuatiliaji, uchambuzi na tathmini ili kubaini matokeo, changamoto na hatua stahiki za kuchukua ili kuleta matokeo tarajiwa. Matokeo ya tathmini na uchambuzi huo yameainishwa katika Taarifa ya Mwaka ya Utekelezaji wa MKUKUTA-II, 2013/14 na Taarifa ya Utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo ya Millenia, 2014. Aidha, kwa mara ya kwanza, Tanzania imeandaa na kutoa Taarifa ya Maendeleo ya Binadamu ya mwaka 2014 inayojulikana kama Tanzania Human Development Report 2014. Taarifa hii inatoa 34 uchambuzi wa kina wa maendeleo na ustawi wa watu kwa kupima na kulinganisha mafanikio kwa vipindi tofauti na baina ya mikoa. 46. Mheshimiwa Spika, baadhi ya mafanikio ya utekelezaji wa MKUKUTA II ni pamoja na kukua kwa uchumi wa Tanzania na wastani wa pato la mwananchi kwa asilimia 7 na asilimia 8.9 kwa mtiririko huo, kwa mwaka 2014. Aidha, umaskini wa kipato umepungua kutoka asilimia 34.4 mwaka 2007 hadi asilimia 28.2 mwaka 2012. Katika eneo la huduma za jamii, yapo mafanikio yaliyopatikana ikiwa ni pamoja na kuongezeka kwa kiwango halisi cha uandikishaji (net enrollment rate) katika elimu ya msingi kutoka asimilia 89.7 mwaka 2013 hadi asilimia 90.2 mwaka 2014. Mafanikio mengine nitayaeleza katika muhtasari wa mafanikio ya jumla ya miaka mitano iliyopita. Sekta ya Fedha 47. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2014/15, Serikali inaendelea kutekeleza Programu ya Maboresho ya Sekta ya Fedha ili kuhakikisha kuwa wananchi wengi wanapata na kutumia 35 huduma zilizo rasmi za fedha kwa lengo la kupunguza umaskini na kukuza Pato la Taifa. Hadi kufikia Desemba 2014, mikopo iliyotolewa kwa sekta binafsi ilifikia shilingi trilioni 12.4 sawa na asilimia 20.9 ya Pato la Taifa. Sehemu kubwa ya mikopo hiyo ilielekezwa kwenye shughuli za biashara iliyopata asilimia 21.7 ya mikopo yote; matumizi binafsi asilimia 15.8; viwanda asilimia 11.8; na kilimo asilimia 8.9. 48. Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kuweka mazingira mazuri ya kisera na kisheria katika Sekta ya Fedha ambapo Sheria ya Mfumo wa Taifa wa Malipo ya mwaka 2015 itakayosimamia na kudhibiti miamala ya malipo ya kielektroniki itaanza kutumika. Aidha, rasimu ya Sera ya Taifa ya Huduma Ndogo Ndogo za Fedha na Mkakati wa Utekelezaji wake imeandaliwa ili kuongeza upatikanaji na utumiaji wa huduma ndogo ndogo za fedha kwa mtu mmoja mmoja, kaya na kwa wajasiriamali wa kipato cha chini. Vilevile, Mfuko wa kutoa mikopo midogo midogo kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za wananchi wenye kipato cha chini umeanzishwa (Housing Micro finance Fund). 36 49. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2015/16 Serikali itapitia na kuandaa utaratibu wa kuziwekea bima mali zake zote kwenye Shirika la Bima la Taifa. Utekelezaji wa suala hili utasaidia kulifufua Shirika la Bima la Taifa na hivyo kuliwezesha kuchangia katika Mfuko Mkuu wa Serikali. Aidha, utaratibu huu utatekelezwa na Serikali kuu na taasisi zake zote pamoja na Mamlaka za Serikali za Mitaa. Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi 50. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2014/15, Serikali imeibua na kuchambua miradi mbalimbali ikiwa katika hatua tofauti za utekelezaji wa miradi hiyo kwa utaratibu wa Ubia. Hadi Aprili 2015, miradi ifuatayo ilitambuliwa na kuchambuliwa kabla ya aidha kuidhinishwa au ushauri kutolewa kwa nia ya kuiboresha. Miradi hiyo ni pamoja na: Mradi wa mabasi yaendayo Kasi Dar es Salaam (DART); mradi wa ujenzi wa Barabara ya Tozo kutoka Dar es Salaam hadi Chalinze; mradi wa kufua umeme wa Kinyerezi III; mradi wa kuzalisha madawa muhimu unaosimamiwa na Bohari 37 Kuu ya Madawa; na mradi wa upanuzi wa Bandari ya Dar es Salaam. Aidha, Serikali kwa mara ya kwanza imeidhinisha taarifa ya upembuzi yakinifu wa mradi wa DART na sasa mradi huu upo katika hatua ya kumpata Mbia Mwendeshaji (Operator). 51. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2015/16, Serikali imedhamiria kuendelea kuimarisha program ya PPP hapa nchini. Miradi ambayo imeidhinishwa itaendelezwa. Aidha, Serikali itaendelea kutoa mafunzo kwa watendaji na wadau mbalimbali katika ngazi mbalimbali ikiwemo Mamlaka za Serikali za Mitaa pamoja na sekta binafsi. Vilevile, Serikali itaendesha warsha na kutoa elimu kwa wadau mbalimbali kuhusu utekelezaji wa dhana ya ubia kati ya sekta binafsi na ya umma. Deni la Taifa 52. Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kusimamia Deni la Taifa kwa kuzingatia Sheria ya Mikopo, Dhamana na Misaada SURA 134. Aidha, msisitizo umewekwa kukopa mikopo yenye masharti nafuu tofauti na ile ya kibiashara ambayo inakopwa kwa 38 uangalifu na kutumika kwenye miradi yenye vichocheo vya ukuaji wa uchumi, ikiwemo ujenzi wa miundombinu ya barabara na reli, ujenzi wa mitambo ya kufua umeme pamoja na ujenzi wa viwanja vya ndege. 53. Mheshimiwa Spika, hadi Machi, 2015, Deni la Taifa likijumuisha deni la ndani na la nje la Serikali pamoja na deni la nje la sekta binafsi lilifikia dola ya Marekani bilioni 19.5 sawa na shilingi trilioni 35 ikilinganishwa na dola za Marekani bilioni 18.7 sawa na shilingi trilioni 30.6 Machi 2014, ikiwa ni sawa na ongezeko la asilimia 21. Kati ya kiasi hicho, deni la nje ni shilingi trilioni 25.6 sawa na asilimia 73.2 ya Deni la Taifa na deni la ndani ni shilingi trilioni 9.4 ambazo ni sawa na asilimia 26.8 ya Deni la Taifa. Ongezeko la Deni la Taifa limetokana na uhitaji wa mikopo mipya yenye masharti nafuu na ya kibiashara iliyoelekezwa kugharamia miradi ya maendeleo, kushuka kwa thamani ya shilingi dhidi ya dola ya Marekani na malimbikizo ya riba ya deni la nje hasa kwenye nchi zisizo wanachama wa Kundi la Paris ambazo Serikali bado inajadiliana nazo ili kupata msamaha wa madeni kulingana na makubaliano na kundi hilo. 39 Hatua iliyofikiwa katika Kukamilisha Zoezi la Nchi Kufanyiwa Tathmini ya Kukopa na Kulipa Madeni 54. Mheshimiwa Spika, majadiliano kati ya Serikali na Kampuni za Moody na Fitch Ratings zitakazofanya kazi ya kutathmini uwezo wa kukopa katika masoko ya fedha ya kimataifa yamekamilika. Ni matumaini yetu kwamba, mikataba baina ya Serikali na Makampuni hayo itasainiwa kabla ya Julai, 2015. Mafanikio ya Utekelezaji wa Bajeti kwa Mwaka 2014/15 55. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2014/15, Serikali imefanikisha upatikanaji wa fedha kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli mbalimbali ikiwa ni pamoja na usambazaji wa umeme na maji vijijini; miundombinu ya usafirishaji (barabara, reli, bandari, na viwanja vya ndege) pamoja na mradi wa bomba la gesi na vinu vya kuchakata gesi; kufanikisha upatikanaji wa fedha kwa ajili ya ununuzi wa chakula cha hifadhi ya Taifa ambapo tani 289,122.3 za 40 nafaka zimenunuliwa; kufanikisha Bunge Maalum la Katiba hadi kupata Katiba inayopendekezwa; kugharamia mikopo ya wanafunzi; kugharamia uchaguzi wa Serikali za Mitaa; Kugharamia uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura na maandalizi ya Uchaguzi Mkuu; na kugharamia ununuzi wa jengo la Ubalozi wa Tanzania nchini Ufaransa. 56. Mheshimiwa Spika, pamoja na Serikali kuendelea kusimamia utekelezaji wa bajeti katika kipindi hicho, bado kuna changamoto mbalimbali za kibajeti kama ifuatavyo:- (i) Ukwepaji wa kodi unaofanywa na wafanyabiashara wasiowaaminifu; (ii) Mchakato mrefu wa upatikanaji wa mikopo ya kibiashara kutoka nje na mabadiliko ya mara kwa mara katika soko la fedha la nje; (iii) Mashirika mengi ya Umma kuendelea kutegemea bajeti ya Serikali kama vile TANESCO, ATCL, TRL na TAZARA 41 na hivyo kuongeza gharama ambazo zingepaswa kulipwa na mashirika yenyewe kama yangekuwa yanajiendesha kwa faida; (iv) Mahitaji makubwa ya fedha kwa ajili ya kuboresha miundombinu hususan ya maji, reli, bandari, viwanja vya ndege na barabara ili kukuza uchumi na kuongeza ajira; (v) Msukosuko wa uchumi duniani umeendelea kuathiri sekta mbalimbali za uchumi hasa kwenye uwekezaji, utalii na upatikanaji wa mikopo katika masoko ya kifedha; (vi) Mabadiliko ya Tabia Nchi ambayo yamesababisha maafa mbalimbali yakiwa ni pamoja na uharibifu wa miundombinu ya usafirishaji; ukosefu wa chakula; ukosefu wa umeme unaozalishwa kwa nguvu za maji; na upotevu wa fursa za ajira; 42 (vii) Kuimarika kwa dola ya Marekani dhidi ya sarafu mbalimbali, kumeongeza gharama za uagizaji wa bidhaa na huduma kutoka nje; na (viii)Kubadilika mara kwa mara kwa bei ya nishati ya mafuta kumekuwa kunachangia kuongeza gharama za uzalishaji na bei ya bidhaa mbalimbali za walaji. 57. Mheshimiwa Spika, Serikali ilichukua hatua mbalimbali ili kukabiliana na changamoto mbalimbali zilizoelezwa hapo juu. Hatua hizi nimezieleza katika maelezo yangu ya awali. Mafanikio na changamoto ya Utekelezaji wa Bajeti kwa Miaka Mitano (2010/11-2014/15) 58. Mheshimiwa Spika, kama nilivyoeleza hapo awali kuwa Bajeti hii ni ya kipekee kwa kuwa ni ya mwisho katika utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2010, naomba kuchukua 43 fursa hii kueleza kwa kifupi mafanikio yaliyopatikana kutokana utekelezaji wa Bajeti kwa miaka mitano iliyopita. 59. Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kutenga fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali chini ya Mpango wa Kwanza wa Maendeleo wa Miaka Mitano na Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umaskini - MKUKUTA. Utekelezaji wa mipango hii umeleta mafanikio makubwa katika sekta mbalimbali za uchumi wetu. Baadhi ya maeneo yaliyopata mafanikio na ufanisi ni pamoja na sekta za nishati, uchukuzi, na kilimo. Kwa kifupi naomba nilieleze Bunge lako Tukufu mafanikio kadhaa yaliyopatikana chini ya mipango hiyo kwa kipindi cha miaka mitano katika sekta nilizozitaja. Miundombinu 60. Mheshimiwa Spika, katika eneo la miundombinu, Serikali imekamilisha ujenzi wa bomba la gesi kutoka Mtwara hadi Dar es Salaam; kujenga vinu vya kuzalisha umeme kwa gesi katika vituo vya Ubungo II megawati 105, Somanga Fungu megawati 7.5 44 pamoja na mtambo wa kutumia mafuta mazito Mwanza megawati 60. Uwekezaji huu, umesaidia kuongeza upatikanaji wa nishati ya umeme kutoka megawati 788.68 mwaka 2010 hadi megawati 1,226.3 mwaka 2014. Aidha, usambazaji wa umeme vijijini umeongezeka kupitia Wakala wa Umeme Vijijini (REA), na hivyo kuongeza idadi ya wananchi wanaopata huduma ya umeme kutoka asilimia 7 mwaka 2011 hadi asilimia 36 mwaka 2014. 61. Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuboresha miundombinu ya barabara na uchukuzi ambapo ujenzi wa barabara na madaraja katika miji mbalimbali pamoja na barabara za kuunganisha mikoa ulikamilika, zikiwemo barabara kutoka Tunduma hadi Sumbawanga, Dodoma hadi Manyoni; Ndundu hadi Somanga na ujenzi wa Daraja la Kikwete katika mto Malagarasi mkoani Kigoma. Aidha, Serikali imeendelea na jitihada za kuboresha sekta ya anga kwa kuendelea na ujenzi na uendelezaji wa viwanja vya ndege ikiwamo upanuzi wa uwanja wa ndege wa kimataifa wa Mwalimu J.K. Nyerere, Viwanja wa ndege Songwe, Mpanda, Kigoma, Tabora, Mafia na Arusha. Vilevile, ukarabati wa 45 miundombinu ya reli na ununuzi wa mabehewa na vichwa vya treni kwa reli ya kati na TAZARA umefanyika. Kilimo 62. Mheshimiwa Spika, katika sekta ya kilimo, Serikali imeendelea kugharamia shughuli mbalimbali na mafanikio yamepatikana katika maeneo kadhaa yakiwemo, kuongezeka kwa ruzuku za pembejeo za kilimo; kuongezeka kwa upatikanaji wa mbegu bora; kuongezeka kwa matumizi ya mbolea kwa wakulima; kuongezeka kwa maafisa ugani wa kilimo na mifugo; ongezeko la ununuzi wa chakula cha hifadhi kutoka kwa wakulima; na uwekezaji katika mashamba kupitia mpango wa SAGCOT. Huduma za Jamii 63. Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuboresha huduma za afya kwa kugharamia ujenzi, ukarabati na upanuzi wa vituo vya afya na hospitali za rufaa za mikoa zikiwemo Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mbeya, Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Singida 46 na Hospitali ya Saratani ya Ocean Road. Kwa upande wa elimu, Serikali imeongeza mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu kufikia shilingi bilioni 1,497.52 ambayo imewanufaisha wanafunzi 211,180. Aidha, idadi ya walimu wa shule za msingi iliongezeka kutoka walimu 165,856 mwaka 2010/11 hadi walimu 190,957 mwaka 2014/15 ambapo ufaulu umeongezeka kutoka asilimia 53.5 mwaka 2010 hadi asilimia 56.9 mwaka 2014. Usimamizi wa Uchumi 64. Mheshimiwa Spika, uchumi umeendelea kukua mwaka hadi mwaka ambapo mwaka 2010 ulikua kwa asilimia 6.4 na unategemewa kukua kwa asilimia 7.3 mwaka 2015. Kwa upande wa mwenendo wa bei, mfumuko wa bei umeendelea kushuka kutoka asilimia 5.6 Desemba, 2010 hadi asilimia 4.5 Aprili, 2015. Aidha, ukuaji wa uchumi umeambatana na ongezeko la ajira 274,030 kwa mwaka 2012/13, ajira 630,616 kwa mwaka 2013/14 na ajira 574,040 kwa mwaka 2014/15. Kutokana na ukuaji huo wa uchumi, Pato la Taifa limekua hadi kufikia shilingi trilioni 79.4 na wastani wa pato la kila mtu limekuwa shilingi 1,724,416 wastani 47 wa dola za Marekani 1,066 kwa mwaka 2014. Hii ina maana kwamba, Tanzania itakuwa ni nchi yenye kipato cha kati ifikapo mwisho wa mwaka huu ikiwa ukuaji huo utakuwa kama ilivyo hivi sasa. Vilevile, uwekezaji kutoka nje uliongezeka kutoka dola za Marekani bilioni 1.2 mwaka 2011 hadi kufikia dola za Marekani bilioni 2.13 kwa mwaka 2013. Thamani ya shilingi 65. Mheshimiwa Spika, thamani ya shilingi ambayo ilikuwa tulivu dhidi ya dola kwa takriban miaka mitatu kuanzia 2012, ilipungua kwa kasi zaidi, hususan kuanzia robo ya mwisho ya 2014. Kushuka huku kumetokana kwa kiasi kikubwa na kuimarika kwa Dola ya Marekani dhidi ya fedha nyingine nyingi duniani kote. Kuimarika kwa dola ya Marekani kumetokana na hali ya uchumi wa Marekani kuwa mzuri hivyo, wawekezaji wanakimbilia kuwekeza zaidi kwenye dola ya Marekani. Aidha, sababu nyingine zilizochangia kutetereka kwa thamani ya Shilingi ya Tanzania ni pamoja na:- 48 (i) Mapato yetu kutokana na mauzo nje ya nchi kuwa madogo kulinganisha na mahitaji yetu ya kununua bidhaa na huduma kutoka nje ya nchi. (ii) Kushuka kwa bei ya dhahabu katika soko la dunia hali ambayo imeathiri mapato yetu yatokanayo na dhahabu kwa kiasi kikubwa. (iii) Kuongezeka kwa mahitaji ya dola kwa ajili ya malipo ya gawio nje ya nchi kwa baadhi ya makampuni binafsi. 66. Mheshimiwa Spika, napenda kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge na wananchi wote kuwa Serikali inachukua hatua muhimu za kuhakikisha thamani ya shilingi yetu inaendelea kuimarika. Hatua hizi ni pamoja na kuimarisha Maeneo Maalum ya Kuzalisha Bidhaa za Kuuza Nje (Export Processing Zones) na Maeneo Maalum ya Uwekezaji Kiuchumi 49 (Special Economic Zones). Hivyo ni rai yetu kwa Watanzania kuzitumia fursa hizi ili kuongeza mauzo yetu nje sambamba na kupunguza uagizaji wa bidhaa na huduma zisizo za lazima kutoka nje ili thamani ya shilingi yetu iendelee kuimarika. Usimamizi wa matumizi 67. Mheshimiwa Spika, katika usimamizi wa matumizi, Serikali imeimarisha mfumo wa malipo kwa kutumia mtandao (TISS) ambapo kwa sasa malipo yanalipwa moja kwa moja kwenye akaunti za walipwaji tofauti na utaratibu wa zamani wa kutumia hundi. Mfumo huu wa malipo unaotumika kwa Wizara, Taasisi pamoja na sekretarieti zote za mikoa unarahisisha malipo kufanyika kwa haraka na kupunguza gharama za miamala.

III. USHIRIKIANO WA KIKANDA 68. Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Jumuiya ya Afrika Mashariki napenda kutoa taarifa kwamba utekelezaji wa mpango kazi wa Itifaki ya Umoja wa Fedha wa Jumuiya ya Afrika Mashariki 50 umeanza baada ya Itifaki hiyo kuridhiwa na Bunge lako tukufu mwezi Juni, 2014. Hadi sasa Jumuiya ya Afrika Mashariki iko kwenye hatua za awali za kuandaa rasimu ya muswada wa sheria ya kuanzisha Taasisi ya Fedha ya Afrika Mashariki (East African Monetary Institute) itakayofanya maandalizi ya kuanzisha Umoja wa Fedha. Taasisi nyingine zitakazoundwa ni pamoja na kamisheni ya kusimamia huduma za fedha, taasisi ya takwimu, taasisi ya kufuatilia na kusimamia utekelezaji wa matakwa ya Itifaki ya Umoja wa Fedha ili kuhakikisha kuwa Jumuiya inaunda umoja wa fedha tulivu, endelevu na stahimilivu. Aidha, Serikali inaendelea kukamilisha utekelezaji wa Itifaki ya Umoja wa Forodha na Itifaki ya Soko la Pamoja kama msingi wa kujenga uchumi imara utakaopelekea kuunda Umoja wa Fedha tulivu na stahimilivu. 69. Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Africa (SADC) ambayo Tanzania ni mwanachama naomba kutoa taarifa kuwa utekelezaji wa mpango kazi wa Itifaki ya Fedha na Uwekezaji ambayo iliridhiwa 51 na Bunge lako Tukufu Juni, 2014 unaendelea. Aidha, nchi wanachama wa SADC zitaanza kutekeleza Mpango Mkakati wa miaka mitano (The Revised Regional Indicative Strategic Development Plan 2015 – 2020) ulioridhiwa na wakuu wa nchi wa Jumuiya hiyo Aprili, 2015. Mpango huo ambao utaongoza utekelezaji wa programu za SADC kwa kipindi cha miaka mitano umeweka vipaumbele katika maeneo ya mtangamano katika maendeleo ya viwanda na masoko; uendelezaji wa miundombinu inayounganisha nchi wanachama; ulinzi na usalama katika ukanda wa SADC; na programu maalum za kikanda. IV. BAJETI YA MWAKA 2015/16 70. Mheshimiwa Spika, kama nilivyoeleza kwenye utangulizi, huu ni mwaka wa kukamilisha mipango tuliyokuwa tumepanga kutekeleza na kujiwekea malengo ya miaka mitano ijayo. Sambamba na Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2015/16, Bajeti hii itaweka kipaumbele katika kugharamia Uchaguzi Mkuu, kuweka msukumo maalum kwenye miradi ya 52 umeme vijijini, maji vijijini, kukamilisha miradi ya kimkakati inayoendelea pamoja na kuwekeza kwenye rasilimali watu. Shabaha na Misingi ya Bajeti kwa Mwaka 2015/16 71. Mheshimiwa Spika, shabaha na malengo ya uchumi jumla katika kipindi cha mwaka 2015/16 ni kama ifuatavyo:- (i) Kuongeza kasi ya ukuaji wa Pato halisi la Taifa kufikia asilimia 7.2 mwaka 2015; (ii) Kuendelea kudhibiti kasi ya mfumuko wa bei na kuhakikisha kuwa unabaki kwenye wigo wa tarakimu moja; (iii) Kuongeza ukusanyaji wa mapato ya ndani ikijumuisha mapato ya mamlaka za serikali za mitaa kufikia asilimia 14.8 ya Pato la Taifa; 53 (iv) Kuongeza mapato ya kodi kufikia asilimia 13.1 ya Pato la Taifa; (v) Matumizi ya serikali yanatarajiwa kuwa asilimia 20.6 ya Pato la Taifa; (vi) Kuwa na nakisi ya bajeti (ikijumuisha misaada) ya asilimia 4.2 ya Pato la Taifa; (vii) Kudhibiti ongezeko la ujazi wa fedha kwa tafsiri pana zaidi (M3) katika wigo wa asilimia 16 kwa mwaka unaoishia Juni 2016; (viii) Kuwa na akiba ya fedha za kigeni kwa kiwango cha kukidhi mahitaji ya uagizaji wa bidhaa na huduma kutoka nje kwa kipindi kisichopungua miezi minne; 54 (ix) Kukamilisha mikataba baina ya Serikali na kampuni za kufanya tathmini (Rating Agencies) kabla ya mwisho wa Julai, 2015; (x) Kuendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji kwa lengo la kuvutia uwekezaji kwa ujumla ikiwa ni pamoja na uwekezaji wa ubia kati ya sekta binafsi na sekta ya umma;na (xi) Kuhakikisha utulivu wa thamani ya shilingi ya Tanzania. 72. Mheshimiwa Spika, misingi ya Bajeti ya Serikali ya mwaka 2015/16 ni kama ifuatavyo:- (i) Kuendelea kuwepo kwa amani, usalama, utulivu na utangamano nchini na nchi jirani; (ii) Kuwepo kwa utulivu wa kiuchumi ndani na nje ya nchi; na 55 (iii) Kuwepo kwa hali nzuri ya hewa nchini na katika nchi jirani itakayowezesha uzalishaji mzuri wa mazao ya chakula na biashara. SERA ZA MAPATO 73. Mheshimiwa Spika, katika maelezo yangu ya awali niliainisha hatua mbalimbali ambazo Serikali itachukua kuimarisha makusanyo ya mapato. Katika hatua mbalimbali za kuboresha ukusanyaji wa mapato pamoja na hatua mpya Serikali inatarajia kukusanya katika mwaka 2015/16 kiasi cha shilingi bilioni 22,495.5. Mapato ya ndani 74. Mheshimiwa Spika, Sera za mapato ya ndani katika mwaka 2015/16, zinalenga kukusanya mapato ya kodi na yasiyo ya kodi ya shilingi bilioni 13,475.6 sawa na asilimia 14.3 ya Pato la Taifa. Kati ya kiasi hicho, mapato ya kodi ni shilingi bilioni 56 12,363 na mapato yasiyo ya kodi ni shilingi bilioni 1,112.7. Mapato yanayotokana na vyanzo vya Halmashauri ni shilingi bilioni 521.9 sawa na asilimia 0.6 ya Pato la Taifa. Maendeleo Katika Sekta ya Gesi 75. Mheshimiwa Spika, kwa miaka ya hivi karibuni kumekuwepo na ugunduzi wa kiwango kikubwa cha gesi kiasi cha takribani futi za ujazo trilioni 55.08 ambacho kinategemewa kuliingizia Taifa mapato katika miaka ijayo. Kuna mategemeo makubwa kutoka kwa wananchi kwamba mapato haya yataleta mchango mkubwa katika maendeleo ya nchi ikiwa ni pamoja na kuongeza ajira kwa watanzania. Hata hivyo, usimamizi wa mapato ya mafuta na gesi una changamoto zifuatazo:- (i)Upatikanaji wa mapato stahiki kutoka katika maeneo yote ya mafuta na gesi; 57 (ii) Kuhakikisha viashiria vya uchumi jumla na sera za kibajeti vinakuwa imara na uchumi hauathiriwi na mabadiliko ya bei na kiasi cha uzalishaji ambavyo huikumba sekta hii mara kwa mara; (iii) Kuhakikisha uwepo wa mapato pindi rasilimali hizo zitakapofikia ukomo; (iv) Kuhakikisha kuwa serikali inabaki katika misingi na ukomo wa bajeti iliyoidhinishwa kwa kuzingatia uhimilivu wa uchumi; (v) Kuhakikisha mapato ya mafuta na gesi hayatumiki kujipatia maslahi binafsi, na hayakumbwi na vitendo vya rushwa, wizi na ubadhirifu. 76. Mheshimiwa Spika, ili kukabiliana na changamoto hizo, Serikali imeandaa Sera ya Usimamizi wa Mapato ya Mafuta na Gesi inayokusudia kuweka mazingira mazuri ya kuhakikisha kuwa kila 58 Mtanzania wa kizazi cha sasa na kijacho ananufaika na mapato yatokanayo na sekta hii. Sera hii imepitishwa Mwezi Mei, 2015. Aidha, Sera hii imetoa mwongozo wa kuanzisha Mfuko wa Mapato ya Mafuta na Gesi utakaoitwa “Oil and Gas Fund” na kuongozwa na mwongozo maalum wa kibajeti “fiscal rules”. Vilevile, Mfuko huo utaweka ukomo wa matumizi ya mapato hayo katika Bajeti ya Serikali na akiba kuhifadhiwa kwenye mfuko huo ili kuhakikisha kiasi kinachopangwa kutumika nchini kinahimiliwa na uchumi. Maandalizi ya kutunga Sheria ya kusimamia mapato hayo yameanza na Muswaada unatarajiwa kuwasilishwa Bungeni hivi karibuni.

V. MABORESHO YA MFUMO WA KODI, ADA, TOZO NA HATUA NYINGINE ZA KODI 77. Mheshimiwa Spika, napenda sasa kuwasilisha mapendekezo ya kufanya marekebisho ya mfumo wa kodi, ikiwemo kurekebisha baadhi ya viwango vya kodi, tozo zisizo za kodi chini ya sheria mbalimbali na kuboresha taratibu za 59 ukusanyaji na usimamizi wa mapato ya Serikali. Marekebisho hayo yanahusu sheria zifuatazo:- a. Sheria ya Kodi ya Mapato, SURA 332; b. Sheria ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi, SURA 82; c. Sheria ya Kodi ya Mauzo ya Nje, SURA 196; d. Sheria ya Uwekezaji Tanzania, SURA 38; e. Sheria ya Forodha ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, ya mwaka 2004; f. Sheria ya Michezo ya Kubahatisha, SURA 41; g. Sheria ya Mafuta ya Petroli SURA 392; 60 h. Sheria ya Ushuru wa Mafuta na Barabara, SURA 220; i. Sheria ya Msajili wa Hazina (Mamlaka na Majukumu) SURA 370; j. Sheria ya Benki Kuu, SURA 197; k. Marekebisho madogo madogo katika baadhi ya sheria za kodi na sheria nyingine mbalimbali; l. Marekebisho ya ada na tozo mbalimbali zinazotozwa na Wizara, Mikoa na Idara zinazojitegemea; (A) Sheria ya Kodi ya Mapato, SURA 332 78. Mheshimiwa Spika, napendekeza kufanya marekebisho kwenye Sheria ya Kodi ya Mapato, SURA 332 kama ifuatavyo:- 61 (i) Kufanya marekebisho ya Sheria ya Kodi ya Mapato ili kuondoa msamaha wa kodi kwenye miradi ya Serikali inayotekelezwa kutokana na mikataba baina ya Serikali na Taasisi mbalimbali inayohusisha mikopo ya kibiashara (non concessional loans). Hatua hii haitahusisha misamaha ya kodi iliyobainishwa kwenye mikataba iliyosainiwa baina ya Serikali na Taasisi mbalimbali kabla ya tarehe 1 Julai 2015 ili kulinda makubaliano hayo. (ii) Kuondoa kodi kwenye mapato yanayotokana na mauzo ya hatifungani zitakazotolewa na Benki ya Maendeleo ya Afrika Mashariki katika Soko la Mitaji la Tanzania hususan katika malipo ghafi yatakayofanywa na walionunua hatifungani hizo. Hatua hii inatarajiwa kuongeza uwezo wa Benki hiyo wa kutoa mikopo nafuu ya uwekezaji kwenye miradi mbalimbali ya maendeleo hapa nchini kama vile kuendeleza miundombinu, nishati, n.k; 62 (iii) Kupunguza kiwango cha chini cha kutoza kodi ya mapato ya ajira kutoka asilimia 12 hadi asilimia 11. Aidha, imekuwa ni dhamira ya Serikali kuwapunguzia mzigo wa kodi wafanyakazi. Ili kutekeleza azma hiyo, Serikali imeendelea kupunguza kiwango cha kodi ya mapato ya ajira kutoka asilimia 18.5 mwaka 2006/07 hadi kufikia asilimia 11 inayopendekezwa sasa. (iv) Kupunguza kiwango cha kutozwa kodi kwenye mapato ghafi ya wafanyabiashara wadogo kwa asilimia 25 ili kuhamasisha ulipaji wa kodi kwa hiari. Hatua hizi za Kodi ya Mapato zinatarajiwa kuongeza mapato ya Serikali kwa kiasi cha shilingi milioni 47,212.2. 63 (B) Sheria ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi, SURA 82; 79. Mheshimiwa Spika, napendekeza kurejesha msamaha wa tozo ya ufundi stadi kwa sekta ya kilimo ili kutoa unafuu wa kodi kwenye shughuli za kilimo mashambani ambazo hutegemea nguvukazi kwa kiasi kikubwa kabla ya kuanza kupata manufaa kutokana na uwekezaji kwenye kilimo. (C) Sheria ya Kodi ya Mauzo ya Nje, SURA 196; 80. Mheshimiwa Spika, napendekeza kuongeza kiwango cha kodi ya mauzo ya nje (export tax) inayotozwa kwenye ngozi ghafi zinazosafirishwa kwenda nje ya nchi kutoka asilimia 60 ya thamani ya ngozi inapokuwa bandarini (FOB) au shilingi 600 kwa kilo moja hadi asilimia 80 ya thamani ya ngozi inapokuwa bandarini (FOB) au dola ya Marekani 0.52 kwa kilo moja kutegemea kiwango kipi ni kikubwa. Hatua hii inazingatia makubaliano ya nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki ya kuwianisha viwango vya kodi kwenye ngozi ghafi. Aidha, lengo la hatua hii ni kuzuia biashara ya 64 magendo ya ngozi ghafi na kuhamasisha usindikaji wa ngozi ndani ya ukanda wa Jumuiya ili kuongeza thamani, mapato na ajira. 81. Mheshimiwa Spika, napendekeza pia kutoza kodi ya mauzo ya nje kwa kiwango cha asilimia 10 ya thamani ya ngozi (FOB) zilizosindikwa kwa kiwango cha kati (wet blue leather). Lengo la hatua hii ni kuhamasisha uongezaji thamani wa bidhaa hizi na uwekezaji katika viwanda vya kutengeneza bidhaa za ngozi hapa nchini. Aidha, hatua hii inatarajiwa kuongeza mapato ya Serikali na ajira. Hatua hizi zinatarajiwa kuongeza mapato ya Serikali kwa kiasi cha shilingi milioni 920.6. (D) Sheria ya Uwekezaji Tanzania, SURA 38 82. Mheshimiwa Spika, napendekeza kurekebisha Sheria ya Uwekezaji kama ifuatavyo:- 65 (i) kuondoa mabomba aina ya PVC na HDPE yanayotambulika kwenye HS Code 3917.31.00 katika orodha ya bidhaa zinazotambuliwa kuwa ni za mtaji (Deemed Capital Goods) ambazo hupata msamaha wa kodi hivi sasa kupitia Kituo cha Uwekezaji Tanzania – TIC. Mapendekezo haya yanazingatia kwamba bidhaa hizi hivi sasa zinazalishwa hapa nchini kwa kiasi cha kutosheleza mahitaji. Hatua hii itasaidia kulinda viwanda vinavyotengeneza mabomba ya aina hiyo na hivyo kuchochea ongezeko la ajira na mapato ya Serikali; (ii) kufuta msamaha unaotolewa kupitia Kituo cha Uwekezaji kwenye matela ya kusafirishia mizigo ili kuwawezesha watengenezaji wa matela hapa nchini kuweza kushindana katika soko, kuhamasisha uwekezaji mkubwa wa kutengeneza matela hapa nchini, kuongeza ajira na kuongeza mapato ya Serikali; 66 (iii) Kutambua uwekezaji mahsusi (Special strategic investment). Aidha, hadhi ya uwekezaji mahsusi itatolewa kwa wawekezaji wanaotimiza vigezo vifuatavyo:- a) Kuwa na mtaji wa jumla usiopungua dola za Marekani milioni 300 au kiasi cha shilingi kinacholingana na kiasi cha dola hizo kwa fedha taslimu pamoja na vifaa; b) Mtaji utakaotumika ni lazima upitishiwe kwenye taasisi za kifedha ikiwemo huduma za bima za hapa nchini; c) Kuwa na uwezo wa kutengeneza ajira za moja kwa moja kwa Watanzania zisizopungua 1,500; ikiwa ni pamoja na idadi inayoridhisha katika ngazi za juu za uongozi wa Kampuni; 67 d) Kuwa na uwezo wa kuzalisha fedha za kigeni au kuzalisha bidhaa mbadala wa zile zinazoagizwa nje; Hatua hizi zinatarajiwa kuongeza mapato ya Serikali kwa kiasi cha shilingi milioni 7,965.5. (E) Sheria ya Forodha ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, ya mwaka 2004 83. Mheshimiwa Spika, kikao cha maandalizi ya Bajeti cha Mawaziri wa Fedha wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (Pre-Budget Consultations of EAC Ministers for Finance) kilichofanyika tarehe 11 April 2015 mjini Arusha kilipendekeza marekebisho ya viwango vya Ushuru wa pamoja wa Forodha (EAC Common External Tariff “CET”) kwa mwaka wa fedha wa 2015/16. Mawaziri wa Fedha pia walifanya marekebisho katika Sheria ya Forodha ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC Customs Management Act, 2004). 68 84. Mheshimiwa Spika, maeneo yanayopendekezwa kufanyiwa marekebisho kwenye viwango vya Ushuru wa Pamoja wa Forodha (EAC Common External Tariff) ni yafuatayo:- (i) Kuendelea kutoza Ushuru wa Forodha kwa kiwango cha asilimia 10 badala ya asilimia 35 kwenye ngano inayotambuliwa katika HS code 1001.99.10 na HS code 1001.99.90. Lengo la hatua hii ni kutoa unafuu kwa viwanda na wazalishaji wa bidhaa na vyakula vinavyotumia ngano na kuimarisha utulivu wa bei ya bidhaa zinazozalishwa kwa kutumia ngano hiyo; (ii) Kuongeza ushuru wa vifungashio vya plastiki vya kuwekea dawa ya meno (Plastic tubes) zinazotambuliwa katika HS code 3923.90.20 kutoka asilimia 10 hadi asilimia 25 ili kulinda wazalishaji wa bidhaa hiyo wa ndani ya ukanda wa Jumuiya ya Afrika Mashariki; 69 (iii) Kutoza ushuru wa forodha kwa kiwango cha asilimia 0 badala ya asilimia 25 kwenye malighafi za kutengeneza pasta na tambi (spaghetti) zinazojulikana kama semolina chini ya HS Code 1103.11.00 kwa mwaka mmoja ili kutoa fursa ya kuwekeza katika kutengeneza malighafi hizo zinazotokana na zao la ngano hapa nchini; (iv) Kuendelea kutoza Ushuru wa Forodha wa asilimia 0 badala ya asilimia 10 kwenye malighafi inayotumika katika kutengeneza sabuni (LABSA) inayotambuliwa katika HS code 3402.11.00, HS code 3402.12.00 na HS code 3402.19.00 kwa kipindi kingine cha mwaka mmoja. Hatua hii inalenga katika kuendelea kutoa unafuu kwa viwanda vidogo na vya kati vya kutengeneza sabuni na hivyo kuweza kuongeza uzalishaji na ajira; 70 (v) Kutoza ushuru wa forodha wa asilimia 25 kwenye bidhaa za vyuma zinazotumika katika ujenzi (bars, rods, angles, shapes, and sections) zinavyotambuliwa katika HS code 7213.10.00 na 7213.20.00 kwa kuwa bidhaa hizi sasa zinatengenezwa hapa nchini kwa kiasi cha kukidhi mahitaji. Hatua hii inalenga katika kulinda viwanda vinavyozalisha bidhaa hizo hapa nchini ili viweze kuhimili ushindani katika soko, kukuza ajira na kuongeza mapato ya Serikali; (vi) Kutoza ushuru wa forodha kwa kiwango cha asilimia 0 badala ya asilimia 10 chini ya utaratibu wa “duty remission” katika vijiti vinavyotumika kutengenezea viberiti chini ya HS code 4421.90.10 kwa kipindi cha mwaka mmoja. Lengo la hatua hii ni kupunguza gharama za uzalishaji wa viberiti na kuongeza ajira. Aidha, Sekretarieti ya Jumuiya ya Afrika Mashariki inaendelea kufanya utafiti kwa lengo la kuweka 71 kiwango stahiki cha ushuru wa forodha kwa bidhaa hiyo; (vii) Kutoza ushuru wa forodha kwa kiwango cha asilimia 0 badala ya asilimia 10 katika bidhaa za glucose syrup zinazotambulika chini ya HS code 1702.30.00 ambazo hutumika kutengeneza bidhaa za pipi kwa kuwa bidhaa hii haizalishwi ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki; (viii) Kupunguza ushuru wa forodha unaotozwa kwenye nyuzi zinazotumika katika kutengeneza nyavu za kuvulia samaki zinazotambuliwa katika HS code 5402.61.00 kutoka asilimia 10 hadi asilimia 0. Marekebisho haya yamezingatia kwamba, nyavu za kuvulia samaki hivi sasa hutozwa ushuru wa asilimia 0; 72 (ix) Kuongeza kiwango maalum cha ushuru wa forodha kwenye sukari kutoka dola za Marekani 200 kwa tani moja au asilimia 100 ya thamani ya bidhaa hiyo inapokuwa imefika bandarini (CIF) hadi dola za Marekani 460 kwa kila tani moja au asilimia 100 ya thamani ya bidhaa hiyo inapofika bandarini, kutegemea kiwango kipi ni kikubwa. Marekebisho hayo yanapendekezwa ili kuendana na hali halisi ya ukuaji wa uchumi katika ukanda wa Afrika Mashariki. Lengo la hatua hii ni kulinda viwanda vinavyozalisha sukari hapa nchini dhidi ya ushindani wa sukari inayoingizwa kutoka nje; (x) Kuongeza kiwango maalum cha ushuru wa forodha kwenye mchele kutoka dola za Marekani 200 kwa tani moja au asilimia 75 ya thamani ya bidhaa hiyo inapofika bandarini (CIF) hadi dola za Marekani 345 kwa kila tani moja au asilimia 75 ya thamani ya bidhaa inapofika bandarini, kutegemea kiwango kipi ni 73 kikubwa. Marekebisho haya yanapendekezwa ili kuendana na hali halisi ya ukuaji wa uchumi katika ukanda wa Afrika Mashariki. Lengo la hatua hii ni kulinda wazalishaji wa bidhaa hiyo hapa nchini dhidi ya ushindani wa mchele unaoingizwa kutoka nje ya nchi. (xi) Kutoza ushuru wa forodha wa asilimia 10 badala ya asilimia 25 kwenye mabasi yenye uwezo wa kubeba abiria zaidi ya 25 yanayotambuliwa katika HS code 8702.10.99 na HS code 8702.90.99 ambayo yataagizwa kwa ajili ya mradi wa mabasi wa jiji la Dar es Salaam (Dar Rapid Transport – DRT) kwa mwaka mmoja. 85. Mheshimiwa Spika, Mawaziri wa Fedha wa Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki walifanya pia marekebisho kwenye Sheria ya Forodha ya Jumuiya ya Afrika 74 Mashariki, (EAC-Customs Management Act, 2004) kama ifuatavyo:- (i) Kufanya marekebisho katika Jedwali la Tano la Sheria ya Forodha ya Jumuiya ya Afrika Mashariki linalotoa msamaha wa Ushuru wa Forodha kwa Majeshi ya Ulinzi na Polisi ili kujumuisha Jeshi la Magereza katika msamaha huu. Msamaha huu unahusu bidhaa zinazoagizwa kwa ajili ya matumizi ya kiofisi tu; na (ii) Kuendelea kutoa msamaha wa Ushuru wa Forodha kwenye migahawa ya majeshi kwa kipindi cha mwaka mmoja. Katika kipindi hicho Serikali ya Tanzania imesisitizwa kuangalia njia mbadala katika kutoa unafuu wa gharama za maisha kwa majeshi ya ulinzi. Tayari nchi za wenzetu za Jumuiya ya Afrika Mashariki wameshaondokana na utaratibu huu wa sasa unaotumika hapa nchini katika migahawa na maduka ya Jeshi. Kwa sasa Serikali inaendelea kutafuta njia mbadala ya kutoa unafuu katika maduka na 75 migahawa ya jeshi. Lengo la hatua hii ni kuhakikisha misamaha inanufaisha walengwa yaani wanajeshi na kwamba wajanja wachache hawaendelei kunufaika na misamaha hiyo. 86. Mheshimiwa Spika, katika kikao cha maandalizi ya Bajeti cha Mawaziri wa Fedha wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (PreBudget Consultations of EAC Ministers for Finance) kilichofanyika tarehe 3 Mei 2014 jijini Nairobi, nchi wanachama zilikubaliana kuanzisha Tozo ya Kuendeleza Miundombinu (infrastructure levy) ya asilimia 1.5 ya thamani ya bidhaa zinapofika bandarini (CIF). Tozo hiyo itatozwa kwenye bidhaa zinazoingizwa katika Nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki. Ili kutekeleza makubaliano hayo, napendekeza kuanzisha Tozo ya Kuendeleza Reli (Railway Development Levy) itakayotozwa kwa kiwango cha asilimia 1.5 ya thamani ya bidhaa inapofika bandarini (CIF). Aidha, nchi za Kenya, Rwanda na Uganda zilianza kutoza na tayari zimeanza kujenga miundombinu kwa kutumia mapato yatokanayo na tozo hiyo. Hatua hii haitahusisha bidhaa ambazo zinapata msamaha wa 76 ushuru wa forodha chini ya Sheria ya Forodha ya Jumuiya ya Afrika Mashariki. 87. Mheshimiwa Spika, napendekeza kuanzisha utaratibu maalum wa kulipa ushuru wa forodha kwa sukari inayotumika viwandani (Industrial sugar). Sukari inayotumika viwandani hivi sasa hulipiwa ushuru wa forodha wa asilimia 10 badala ya kiwango cha ushuru kilichoainishwa kisheria cha asilimia 100. Katika utaratibu maalum unaopendekezwa, waagizaji watatakiwa kulipia ushuru wa asilimia 50 na mara baada ya kuzalisha bidhaa viwandani na kuthibitishwa na Mamlaka ya Mapato kwamba sukari hiyo imetumika ipasavyo watarejeshewa asilimia 40. Lengo la hatua hii ni kudhibiti matumizi ya sukari inayotumika viwandani, kuepuka sukari hii kuuzwa kama sukari ya kawaida na kuzuia uvujaji wa mapato unaoweza kusababishwa na matumizi mbadala ya sukari hiyo. Hatua hizi kwa pamoja zinatarajiwa kuongeza mapato ya Serikali kwa kiasi cha shilingi milioni 155,447.6 . 77 (F) Sheria ya Michezo ya Kubahatisha, SURA 41 88. Mheshimiwa Spika, napendekeza kufanya marekebisho katika Sheria ya Michezo ya Kubahatisha, SURA 41 ili kufanya yafuatayo:- (i) kutoza kodi ya michezo ya kubahatisha katika zawadi za ushindi kwa kiwango cha asilimia 18 ya zawadi inayotolewa kwa mshindi. Hatua hii inalenga katika kuongeza wigo wa mapato ya Serikali; (ii) kutoza ada ya Leseni Kuu (Principal License) ya dola za Marekani 30,000 au kiasi cha shilingi kinacholingana na hicho kwa uendeshaji wa bahati nasibu ya kutabiri matokeo ya michezo (sports betting); na kutoza ada ya Leseni Kuu ya dola za Marekani 10,000 au kiasi cha shilingi kinacholingana 78 na hicho kwa uendeshaji wa michezo ya Mashine za Kamari (Slot Machines). Lengo la hatua hii ni kuimarisha usimamizi wa michezo hii inayokua kwa kasi na kuongeza wigo wa mapato ya Serikali; (iii) kuweka utaratibu wa kutoa Hati ya Kufaa (certificate of suitability) kwa muombaji ambaye baada ya kupekuliwa na kuonekana kufaa kupewa leseni. Hati hii italipiwa ada ya shilingi 1,000,000; (iv) kuweka utaratibu wa usajili wa vifaa vya michezo ya kubahatisha na kutoza ada ya usajili kama ifuatavyo:- 79 Kifaa Casino Uendeshaji wa Mashine za Kamari (Slot Machines Operations) Kutabiri matokeo ya michezo (Sports Betting) 40-Machine Site Mashine za Kamari (Slot machine) Sh.50,000 Sh.30,000 - Sh.40,000 Live Tables Sh.100,000 - - Electronic Tables – Seat Sh.50,000 - Sh.50,000 Kutabiri matokeo ya michezo (Sports Betting Terminals) - - Sh.30,000 - Ukaguzi wa vifaa hivi utafanyika kila mwaka ili kuwalinda wachezaji na kugundua mashine ambazo hazikidhi viwango. Hatua hizi kwa pamoja zinatarajiwa kuongeza mapato ya Serikali kwa kiasi cha shilingi milioni 12,275.2. 80 (G) Sheria ya Mafuta ya Petroli, SURA 392 89. Mheshimiwa Spika, napendekeza kuongeza Tozo ya Mafuta ya Petroli kwa viwango vifuatavyo:- a) Mafuta ya dizeli kutoka shilingi 50 kwa lita hadi shilingi 100 kwa lita, ikiwa ni ongezeko la shilingi 50 kwa lita; b) Mafuta ya petroli kutoka shilingi 50 hadi shilingi 100 kwa lita, ikiwa ni ongezeko la shilingi 50 kwa lita; c) Mafuta ya taa kutoka shilingi 50 kwa lita hadi shilingi 150 kwa lita, ikiwa ni ongezeko la shilingi 100 kwa lita ili kuondoa uwezekano wa kuchakachua: Hatua ya kuongeza Tozo ya Mafuta ya Petroli inatarajiwa kuongeza mapato ya Serikali kwa kiasi cha shilingi milioni 139,786.8. Fedha hizi zote zitaelekezwa katika mfuko wa REA 81 kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli za usambazaji wa umeme vijijini. 90. Mheshimiwa Spika, napendekeza Waziri wa Fedha apewe mamlaka ya kusamehe Tozo ya Mafuta ya Petroli kwenye miradi inayotekelezwa kwa misaada ya wafadhili na yenye mikataba isiyohusisha utozaji wa tozo hii. Lengo la hatua hii ni kuondoa usumbufu na ucheleweshaji katika utekelezaji wa miradi kutokana na kutokuwepo kwa mamlaka ya kisheria kwa Waziri wa Fedha kutoa msamaha wa tozo hii. (H) Sheria ya Ushuru wa Mafuta na Barabara, SURA 220 91. Mheshimiwa Spika, napendekeza kuongeza Ushuru wa mafuta kwa viwango vifuatavyo:- 82 a) Mafuta ya dizeli kutoka shilingi 263 kwa lita hadi shilingi 313 kwa lita, ikiwa ni ongezeko la shilingi 50 kwa lita; b)Mafuta ya petroli kutoka shilingi 263 kwa lita hadi shilingi 313 kwa lita, ikiwa ni ongezeko la shilingi 50 kwa lita. Hatua ya kuongeza Ushuru wa Barabara inatarajiwa kuongeza mapato ya Serikali kwa kiasi cha shilingi milioni 136,370.2. Napendekeza kuwa, fedha zitakazopatikana kutokana na ongezeko hilo la Ushuru wa barabara zitumike katika kugharamia usambazaji wa umeme vijijini kupitia mfuko wa REA. (I) Sheria ya Msajili wa Hazina (Mamlaka na Majukumu), SURA 370 92. Mheshimiwa Spika, napendekeza kufanya marekebisho kwenye Sheria ya Msajili wa Hazina kwa kuweka ukomo wa matumizi (operating expenditure ceiling) kwa mashirika na taasisi 83 zote za umma zinazojiendesha bila ruzuku ya Serikali. Lengo ni kuweka utaratibu utakaosaidia kudhibiti matumizi na kuyawezesha mashirika na taasisi za Serikali kuchangia ipasavyo kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali. Kwa msingi huo, napendekeza kuweka ukomo usiozidi asilimia 60 ya mapato kutumika katika matumizi ya uendeshaji na asilimia 70 ya bakaa itakayopatikana itawasilishwa katika Mfuko Mkuu wa Serikali. Aidha, napendekeza mashirika na taasisi nyingine zilizokuwa zinachangia asilimia 10 ya mapato ghafi sasa yachangie asilimia 15 katika Mfuko Mkuu wa Serikali. (J) Sheria ya Benki Kuu SURA 197 93. Mheshimiwa Spika, napendekeza kufanya marekebisho kwenye Sheria ya Benki Kuu ili kuiwezesha Serikali kukopa moja ya nane ya mapato ya mwaka mmoja uliopita badala ya kutumia wastani wa mapato ya miaka mitatu ya nyuma. Hatua hiyo inaipa Serikali uwezo zaidi wa kutekeleza bajeti yake. 84 (K) Marekebisho madogo madogo katika baadhi ya Sheria za Kodi na Sheria nyingine mbalimbali 94. Mheshimiwa Spika, napendekeza kufanya marekebisho mengine madogo madogo yasiyo ya kisera katika sheria mbalimbali za kodi pamoja na sheria nyingine mbalimbali ili ziwe sanjari na azma ya kurahisisha utekelezaji wake. Marekebisho hayo yataainishwa katika Muswada wa Sheria ya Fedha ya mwaka 2015. (L) Marekebisho ya Ada na Tozo Mbalimbali za Wizara, Mikoa na Idara zinazojitegemea 95. Mheshimiwa Spika, napendekeza kufanya marekebisho ya viwango vya ada na tozo mbalimbali zinazotozwa na Wizara, Mikoa na Idara zinazojitegemea ili kuvihuisha kulingana na hali halisi ya ukuaji wa uchumi. 85 (M) Tarehe ya Kuanza Kutekeleza Hatua Mpya za Kodi 96. Mheshimiwa Spika, Hatua hizi za kodi zinazopendekezwa zitaanza kutekelezwa tarehe mosi Julai, 2015, isipokuwa pale itakapoelezwa vinginevyo.

 VYANZO VINGINE VYA MAPATO Misaada na Mikopo ya Masharti Nafuu 97. Mheshimiwa Spika, jumla ya misaada na mikopo nafuu inayokadiriwa katika Bajeti ya mwaka 2015/16 ni shilingi bilioni 2,322.5 ambayo ni asilimia 10 ya Bajeti ya Serikali. Naomba kuwatambua na kuwashukuru Washirika wetu wa Maendeleo wanaotarajia kuchangia Bajeti ya Serikali kama ifuatavyo: Nchi za Canada, China, Denmark, Finland, Hispania, India, Ireland, Italia, Japani, Korea ya Kusini, Marekani, Norway, Sweden, Ubelgiji, Ufaransa, Uholanzi, Uingereza, Ujerumani, na Uswisi, pia taasisi mbalimbali za kimataifa ikiwemo Benki ya Maendeleo ya Afrika, 86 Benki ya Dunia, Arab Bank for Economic Development in Afrika (BADEA), Global Fund, Organization of the Petroleum Exporting Countries (OPEC Fund), Saudi Fund, Kuwait Fund, Umoja wa Ulaya, na Mashirika ya Umoja wa Mataifa. Aidha, napenda kutambua uhusiano mzuri tulionao na Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) chini ya Mpango wa Ushauri wa Kisera unaojulikana kama Policy Support Instrument (PSI). Mikopo ya Kibiashara ya Ndani na Nje 98. Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kukopa kutoka katika vyanzo vya ndani na nje ili kugharamia miradi mbalimbali ya maendeleo. Katika mwaka 2015/16, Serikali inategemea kukopa kiasi cha shilingi bilioni 4,033 kutoka katika soko la fedha la ndani kwa utaratibu wa kuuza dhamana za muda mfupi na hatifungani za serikali. Kati ya kiasi hicho, shilingi bilioni 805 ni kwa ajili ya kugharamia miradi ya maendeleo, shilingi bilioni 2,600 ni kwa ajili ya kulipia dhamana na hatifungani za serikali zinazoiva 87 kwa utaratibu wa rollover na shilingi bilioni 628.3 ni kwa ajili ya kulipia madai yaliyohakikiwa. 99. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2015/16, Serikali inategemea kukopa kiasi cha dola za Marekani milioni 1,074 sawa na shilingi bilioni 2,142.5 kwa masharti ya kibiashara kutoka kwenye masoko ya fedha ya kimataifa kwa ajili ya kugharamia miradi mbalimbali ya maendeleo ya kimkakati. Uamuzi wa kukopa kiasi hicho umezingatia viashiria muhimu vya uhimilivu wa Deni la Taifa. SERA ZA MATUMIZI 100. Mheshimiwa Spika, bajeti ya mwaka 2015/16 inalenga katika kukamilisha miradi iliyoanza kutekelezwa na Serikali na kulinda mafanikio yaliyokwishapatikana katika sekta ya Elimu, Afya, Maji na Maendeleo ya Jamii. Hivyo, hakutakuwa na miradi mipya isipokuwa ile tu ambayo majadiliano yake yamefikia katika hatua za mwisho. Miradi inayotegemewa kukamilishwa na 88 imetengewa fedha ni pamoja na upanuzi wa uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere, Ujenzi wa mtambo wa kufua Umeme - Kinyerezi II, Ujenzi wa Maghala yenye uwezo wa kuhifadhi tani 5,000 Wilaya ya Mbozi na tani 10,000 Songea Mjini; Ujenzi wa Mfumo Unganishi wa Kuhifadhi Kumbukumbu za Ardhi (Integrated Land Management Information System); kuimarisha na kuboresha vitendea kazi na huduma katika reli ya kati; Ujenzi wa Bandari Mpya ya Mbegani; Awamu ya tatu ya ujenzi wa Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano; kuendelea na utekelezaji wa Mradi wa Upanuaji wa mtambo wa maji wa Ruvu juu na Ruvu chini; kuandikisha wapiga kura na Vitambulisho vya Taifa. 101. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha 2015/2016 Serikali imekadiria kutumia jumla ya shilingi bilioni 22,495.5 kwa ajili ya matumizi ya kawaida na ya maendeleo. Kiasi hiki kinajumuisha shilingi bilioni 16,576.4 kwa ajili ya matumizi ya kawaida na shilingi bilioni 5,919.1 ni matumizi ya maendeleo. 89 Mgawanyo wa Fedha katika Sekta 102. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2015/16, mgawanyo wa bajeti katika sekta ambao haujumuishi madeni ya kisekta yanayolipwa kupitia Mfuko Mkuu wa Serikali (CFS) ni kama ifuatavyo:- (i) Nishati na Madini: shilingi bilioni 916.7 zimetengwa kwa ajili ya sekta ya nishati sawa na asilimia 5.7 ya bajeti yote bila kujumuisha Mfuko Mkuu wa Serikali. Kati ya kiasi hicho, shilingi bilioni 447.1 zimetengwa kwa ajili ya mradi wa usambazaji wa umeme vijijini; (ii) Miundombinu: shilingi bilioni 2,428.8 zimetengwa kwa ajili ya sekta ya ujenzi na uchukuzi sawa na asilimia 15.1 ya bajeti yote bila kujumuisha Mfuko Mkuu wa Serikali. Kati ya kiasi hicho, shilingi bilioni 322.4 zimetengwa kwa ajili ya miundombinu ya usafirishaji; shilingi bilioni 1,608.5 kwa ajili ya ujenzi na 90 ukarabati wa barabara na madaraja; shilingi bilioni 9.5 kwa ajili ya kujenga na kuboresha bandari; (iii) Kilimo: Jumla ya shilingi bilioni 1,001.4 sawa na asilimia 6.2 ya bajeti yote bila kujumuisha Mfuko Mkuu wa Serikali, zimetengwa kwa ajili ya kuimarisha miundombinu ya umwagiliaji, ujenzi wa maghala na masoko katika maeneo mbalimbali nchini; (iv) Elimu: Jumla ya shilingi bilioni 3,870.2 sawa na asilimia 24.0 ya bajeti yote bila kujumuisha Mfuko Mkuu wa Serikali, zimetengwa kwa ajili ya sekta hii ili kugharamia ubora wa elimu na kuimarisha miundombinu ya elimu Kati ya fedha hizo, shilingi bilioni 348.3 zimetengwa kwa ajili ya kutoa mikopo ya elimu ya juu; (v) Maji: Jumla ya shilingi bilioni 573.5 sawa na asilimia 3.6 ya bajeti yote bila kujumuisha Mfuko Mkuu wa 91 Serikali, zimetengwa kwa ajili ya kuimarisha miundombinu ya maji mijini na vijijini; na (vi) Afya: Jumla ya shilingi bilioni 1,821.1 sawa na asilimia 11.3 ya bajeti yote bila kujumuisha Mfuko Mkuu wa Serikali, zimetengwa kwa ajili ya kuboresha huduma za afya nchini ikiwa ni pamoja na ununuzi wa madawa, kuzuia magonjwa ya mlipuko, chanjo za watoto, ujenzi wa zahanati na kudhibiti UKIMWI na Malaria. Masuala yanayohusu Mamlaka za Serikali za Mitaa 103. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2015/16, Mikoa na Halmashauri zimetengewa shilingi bilioni 4,947.8 ikiwa ni nyongeza ya shilingi bilioni 448.8 ikilinganishwa na Bajeti ya mwaka 2014/15. Aidha, Halmashauri zinakadiriwa kukusanya mapato ya ndani ya shilingi bilioni 521.8. Vilevile, Serikali inaendelea kuziwezesha Halmashauri nchini katika ukusanyaji wa mapato kwa kutumia mifumo ya kielektroniki, uboreshaji wa 92 sheria mbalimbali na kuwajengea uwezo watumishi katika eneo hili ili kuimarisha ukadiriaji na ukusanyaji wa mapato ya ndani. 104. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2015/16, kiasi cha shilingi bilioni 36.5 zimetengwa kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za watumishi pamoja na majengo ya makao makuu ya halmashauri mpya. Aidha, shilingi bilioni 27.2 zimetengwa kwa ajili ya ujenzi wa ofisi na nyumba za Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya, pamoja na Makatibu Tarafa katika maeneo hayo.

VI. SURA YA BAJETI KWA MWAKA 2015/16 105. Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia sera za uchumi jumla pamoja na misingi na shabaha ya bajeti, sura ya bajeti itakuwa kama ifuatavyo; Serikali imepanga kukusanya jumla ya shilingi bilioni 22,495.5 kutoka kwenye vyanzo vya ndani na nje. Mapato ya kodi na mapato yasiyo ya kodi yanatarajiwa kufikia shilingi bilioni 13,475.6 sawa na asilimia 14.3 ya Pato la Taifa. Aidha, mapato kutokana na vyanzo vya Mamlaka za Serikali za Mitaa 93 yanatarajiwa kufikia shilingi bilioni 521.9 sawa na asilimia 0.6 ya Pato la Taifa. 106. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2015/16, Washirika wa Maendeleo wameahidi kuchangia shilingi bilioni 2,322.5 kama misaada na mikopo nafuu. Kati ya fedha hizo, shilingi bilioni 660.3 ni mikopo nafuu ya kibajeti, shilingi bilioni 1,463.2 ni misaada na mikopo nafuu kwa ajili ya miradi ya maendeleo na shilingi bilioni 119 ni Mifuko ya Pamoja ya Kisekta. 107. Mheshimiwa Spika, ili kuziba nakisi ya bajeti, Serikali inatarajia kukopa kutoka katika vyanzo vya ndani na nje shilingi bilioni 6,175.5. Kati ya fedha hizo, shilingi bilioni 2,600 ni kwa ajili ya kulipia hatifungani na dhamana za Serikali zinazoiva; shilingi bilioni 1,433 ni mkopo wa ndani ambao unajumuisha shilingi bilioni 628.3 kwa ajili ya kulipia madeni yaliyohakikiwa na shilingi bilioni 804.7 kwa ajili ya kugharamia miradi ya maendeleo; shilingi bilioni 2,124.5 ni mikopo ya nje yenye masharti ya kibiashara ambayo itatumika kugharamia miradi ya maendeleo. 94 108. Mheshimiwa Spika, Serikali imekadiria kutumia jumla ya shilingi bilioni 22,495.5 kwa ajili ya matumizi ya kawaida na ya maendeleo. Kati ya fedha hizo, matumizi ya kawaida ni shilingi bilioni 16,576.4 ambayo yanajumuisha shilingi bilioni 6,466.5 kwa ajili ya mishahara ya watumishi wa Serikali, Wakala na Taasisi za Serikali; shilingi bilioni 6,396.6 ni kwa ajili ya Mfuko Mkuu wa Serikali, na matumizi mengineyo shilingi bilioni 3,713. Matumizi ya maendeleo ni shilingi bilioni 5,919.1 bila kujumuisha matumizi ya kawaida yenye sura ya kimaendeleo. Aidha, matumizi ya maendeleo ni asilimia 37.4 ya Bajeti yote ambayo inajumuisha matumizi ya kawaida yenye sura ya kimaendeleo yanayolipwa kupitia Mfuko Mkuu wa Serikali. 109. Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia mfumo wa bajeti kama ulivyoelezwa hapo juu, mfumo wa bajeti kwa mwaka 2015/16 unakuwa kama ifuatavyo:- 95 Mapato A. Mapato ya Ndani-Serikali Kuu 13,475,644 (i) Mapato ya Kodi (TRA) 12,362,959 (ii) Mapato yasiyo ya kodi 1,112,685 o/w Mapato ya mauzo ya Gesi Asili 42,060 B. Mapato ya Halmashauri 521,879 C. Mapato na Mikopo kutoka nje 2,322,518 (i) Mikopo ya masharti nafuu 660,337 (ii)Misaada na Mikopo ya Miradi 1,463,155 (iii)Misaada na Mikopo ya Kisekta 199,026 D. Mikopo ya Ndani na yenye Masharti ya Kibiashara 6,175,452 (i)Mikopo-Masharti ya Kibiashara 2,142,469 (ii) Mikopo-asilimia 1.5 ya GDP 1,432,983 (iii)Mikopo- Rollover 2,600,000 JUMLA YA MAPATO YOTE 22,495,493 Matumizi E. Matumizi ya Kawaida 16,576,439 (i)Mfuko Mkuu wa Serikali 6,396,602 o/w Malipo ya mikopo iliyokugharamia miradi ya maendeleo 2,499,499 (ii)Mishahara 6,466,481 (iii)Wizara 3,146,320 (iv)Mikoa 38,273 (v) Mamlaka za Serikali za Mitaa 528,763 F. Matumizi ya Maendeleo 5,919,053 (i)Wizara na Taasisi 5,179,702 (ii)Mikoa 50,906.00 (iii)Mamlaka za Serikali za Mitaa 688,445 JUMLA YA MATUMIZI YOTE 22,495,493 Shilingi Milioni 96

VII. HITIMISHO 110. Mheshimiwa Spika, katika kuhitimisha hotuba yangu napenda kusisitiza mambo sita: Kwanza, Serikali imejizatiti katika ukusanyaji wa mapato ili Bajeti hii itekelezwe kama ilivyopangwa. Hatutamvumilia yeyote atakayekwamisha azma hii ya Serikali. Sisi viongozi tuwe mstari wa mbele katika kulipa kodi na kuhakikisha hatutumii mamlaka na madaraka yetu kusaidia ukwepaji kodi. Pili, ili kuhakikisha Waheshimiwa wabunge kupitia Muhimili wa Bunge wanasimamia utendaji wa mashirika ya umma ipasavyo pamoja na kutekeleza mapendekezo ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali, Waheshimiwa wabunge wote ambao ni Wajumbe wa Bodi za Wakurugenzi wa Mashirika na Taasisi za Umma ujumbe wao utafikia ukomo ifikapo tarehe 30 Juni, 2015. Tatu, Serikali inatambua kero na ugumu unaosababishwa na ulimbikizaji wa madai ya makandarasi, wazabuni na watumishi wa Serikali. Kuanzia mwaka ujao wa fedha Serikali italipa ankara za umeme na maji za Serikali kwa pamoja (Centrally) na fedha hizo 97 zitatoka katika Mafungu husika. Kama nilivyoeleza, Serikali imeanza kukabiliana na tatizo hili na imedhamiria kulishughulikia kwa dhati. Nne, suala la madeni ya mifuko ya Hifadhi ya Jamii linashughulikiwa na litamalizika. Napenda kuwahakikishia Watanzania kuwa Serikali inasimamia mifuko hii kuhakikisha inabaki kuwa himilivu na zaidi ya hapo Serikali iko makini kuhakikisha mafao ya wastaafu wote yanalipwa kwa wakati na kwa ukamilifu. Tano, kama nilivyoeleza Serikali imeongeza kima cha chini cha malipo ya pensheni ya kila mwezi kwa wastaafu kutoka shilingi 50,000 hadi shilingi 85,000 ambalo ni ongezeko la asilimia 70. Hii ni katika jitihada za Serikali kuboresha maisha ya wastaafu. Na Sita, kwa kutambua mchango wa wazee katika Taifa letu, Serikali inakamilisha taratibu za kuwalipa mafao. 98 111. Mheshimiwa Spika, napenda kuchukua fursa hii kuwatakia kila la kheri Waheshimiwa Wabunge wote wanaogombea nafasi mbalimbali za uongozi wakiwemo waliotangaza nia katika Uchaguzi Mkuu. Kwa Watanzania wenzangu wote napenda nichukue fursa hii kuwahamasisha sote tujitokeze kujiandikisha katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura na tushiriki kupiga kura mwezi Oktoba 2015 kwa amani na utulivu. 112. Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja.