Maelezo Kuhusu Kushuka
kwa Thamani ya Shilingi ya Tanzania kwa Kamati ya Fedha Uchumi na Biashara
1. Utangulizi
1.1 Thamani ya Shilingi kwa Kipindi cha Mwaka 2010 mpaka 2014
Thamani ya shilingi ya Tanzania dhidi ya dola ya Marekani
katika soko la jumla la fedha za kigeni (Interbank
foreign exchange market-IFEM) ilishuka kutoka shilingi 1,318 kwa dola moja
mwezi Januari 2010 na kufikia kiwango cha shilingi 1,543 kwa dola moja ya
Marekani mwezi Juni 2011. Katika kipindi hicho thamani ya shilingi katika soko
la rejareja ilishuka kutoka shilingi 1,333 kwa dola moja ya Marekani na kufikia
shilingi 1,547 kwa dola. Kushuka kwa thamani ya shilingi kulichangiwa na mfumuko
mkubwa wa bei pamoja na mauzo hafifu nje ya nchi hasa kufuatia mdororo wa
uchumi duniani.
Thamani ya shilingi ilishuka kwa kasi zaidi kati ya
mwezi Juni 2011 hadi Oktoba 2011 kufuatia baadhi ya washiriki wa soko la fedha
za kigeni kucheza kamari/kufanya biashara ya dola kwa lengo ya kujinufaisha (speculation). Kufuatia hali hii, hatua mbalimbali
zilichukuliwa na Benki Kuu ikiwa ni pamoja na kuongeza viwango vya akiba
ambavyo mabenki yanatakiwa kuhifadhi Benki Kuu (SMR) kutoka asilimia 20 mpaka
asilimia 40 kwa amana za serikali; kupunguza kiwango cha fedha za kigeni ambazo
mabenki yanaruhusiwa kubaki nazo—ambazo zinaweza kutumika kutafuta faida kwa
miamala ya fedha za kigeni (net open
position, NOP)—kutoka asilimia 20 hadi asilimia 10 na hatimaye asilimia 7.5.
Benki kuu pia iliongeza kiwango cha mauzo ya fedha za kigeni kwenye soko la jumla.
Kufuatia juhudi hizo, thamani ya shilingi iliimarika tena na kubaki tulivu kwa
takribani miaka mitatu hadi kufikia robo ya mwisho ya mwaka 2014 (Jedwali Na. 1 na Chati Na. 1a & 1b).
Chati Na 1a: Wastani wa
Mwenendo wa Thamani ya Shilingi dhidi ya
dola ya Marekani
Chati Na 1b: Wastani wa bei ya dola kwa
shilingi - soko la jumla
Kama inavyoonekana katika Chati Na. 2 hapo chini, thamani ya shilingi ilipungua kwa wastani
wa asilimia 8.6 kwa mwaka kati ya Januari 2010 hadi Mei 2011. Baada ya hapo
kasi ya kushuka thamani ilipanda hadi wastani wa asilimia 11.7 kwa mwaka kati
ya Juni 2011 hadi Novemba 2011. Kutokea Desemba 2011 hadi Septemba 2014 thamani
ya shilingi ilitulia ambapo ilipungua kwa wastani wa asilimia 1.8 kwa mwaka.
Chati Na. 2: Mwenendo wa Thamani ya Shilingi dhidi ya dola ya Marekani
2. Thamani ya shilingi kwa kipindi cha Machi 2014 hadi Machi 2015
Katika kipindi cha Machi 2014 hadi Machi 2015,
thamani ya shilingi ilishuka kwa asilimia 9.6 katika soko la jumla na asilimia 13.0
katika soko la rejareja (Jedwali Na. 1).
Kushuka huku kulitokana zaidi na kuimarika kwa uchumi wa Marekani. Kuimarika
kwa uchumi wa Marekani kumefananya wawekezaji wengi duniani kuwekeza zaidi
Marekani na hivyo kuongeza mahitaji ya dola ya Marekani. Kwa sababu hiyo sarafu
za nchi nyingi duniani pia zimeshuka
thamani dhidi ya dola ya Marekani kama inavyoonekana katika Jedwali Na. 2. Baadhi ya sarafu hizo
kama vile Euro ya Ulaya, Pauni ya Uingereza, Yen ya Japan, Shilingi ya Uganda,
na Rand ya Afrika Kusini, zimeshuka kwa kasi zaidi ya shilingi ya Tanzania.
Jedwali Na. 1: Mwenendo
wa Thamani ya Shilingi dhidi ya dola ya Marekani
|
Machi
2014
|
Machi
2015
|
Badiliko
|
Soko la jumla (IFEM)
|
1,629.6
|
1,786.3
|
9.6%
|
Soko la rejareja (bureau-mean rate)
|
1,631.9
|
1,844.5
|
13.0%
|
Jedwali Na 2: Mwenendo
wa Thamani za Sarafu Mbalimbali dhidi ya Dola ya Marekani
|
Machi
2014
|
Machi
2015
|
Badiliko
|
Tanzanian Shilling
|
1,629.60
|
1,786.30
|
9.62%
|
Great Britain Pound
|
0.60
|
0.68
|
12.65%
|
Euro
|
0.73
|
0.93
|
28.27%
|
Japanese Yen
|
103.27
|
119.86
|
16.07%
|
Indian Rupee
|
59.97
|
62.50
|
4.23%
|
Kenyan shilling
|
86.55
|
92.40
|
6.76%
|
Ugandan Shilling
|
2,588.73
|
3,030.32
|
17.06%
|
South African Rand
|
10.57
|
12.18
|
15.26%
|
2.1 Sababu nyingine za kushuka kwa thamani ya shilingi kwa kipindi cha Machi 2014 hadi Machi 2015
2.1.1 Kupungua kwa kasi ya upatikanaji wa dola nchini ukilinganisha na mahitaji
Upatikanaji wa dola nchini umepungua kutokana na sababu
mbalimbali kama zinavyoainishwa hapa chini:
Kupungua kwa mapato ya mauzo nje
ya nchi
Mapato yanayotokana na mauzo ya bidhaa na huduma
nje ya nchi yamekuwa yakiongezeka kwa kiasi kidogo ukilingalisha na mahitaji ya
fedha za kigeni kwa ajili ya kununua bidhaa na huduma kutoka nje ya nchi. Kwa kipindi
cha mwaka unaoishia Machi 2015, mauzo ya bidhaa na huduma nje yalifikia dola za
Marekani milioni 9,355.5 ukilinganisha na uagizaji wa bidhaa na huduma kutoka
nje ambao ulikuwa na thamani ya dola za Marekani milioni 13,456.9.
Eneo mojawapo ambalo mapato yake yamepungua ni mauzo
ya dhahabu kutokana na kushuka kwa bei ya dhahabu katika soko la dunia na
kupungua kwa uzalishaji wa dhahabu nchini. Uzalishaji wa dhahabu ulipungua katika
kipindi hicho kutokana na kufungwa kwa baadhi ya migodi kama Tulawaka na
Resolute. Kwa mwaka unaoishia Machi 2015, mapato kutokana na dhahabu yalishuka hadi
dola za Marekani milioni 1,377.2 kutoka milioni 1,588.9 zilizopatikana katika
mwaka ulioishia Machi 2014. Hali hii imepunguza ahueni ambayo ingeweza kupatikana
kutokana na ongezeko la mauzo ya bidhaa za viwandani pamoja na utalii.
Chati Na. 3: Mwenendo wa Mauzo ya Dhahabu Nje ya Nchi kwa Mwaka Unaoishia Machi (Dola Million)
Ucheleweshwaji
wa fedha kutoka kwa wahisani na mikopo ya kibiashara toka nje ya nchi
Kuanzia
robo ya pili ya mwaka 2014/15, wahisani hawakutoa fedha za kigeni kama
ilivyokuwa imetarajiwa. Katika kipindi cha robo tatu za kwanza za mwaka 2014/15
fedha za wahisani zilizopokelewa zilikuwa dola za Marekani milioni 122
ikilinganishwa na makisio ya dola za Marekani milioni 473.7. Hali hii imechangia katika upungufu wa fedha
za kigeni nchini na pia kuleta hisia ya kuwepo kwa uhaba katika soko la fedha
za kigeni.
Katika
mwaka 2014/15, serikali ilitarajia kupokea mikopo ya kibiashara kutoka nje
yenye thamani ya dola za Marekani milioni 800, lakini hadi mwezi Machi 2015 mikopo
yenye thamani ya dola milioni 310 tu ndiyo iliyokuwa imepatikana. Hali hii pia imechangia
upungufu wa fedha za kigeni nchini.
Chati Na. 4: Mwenendo wa Upatikanaji wa Fedha za Kigeni kwa Bajeti
Msimu wa
mapato madogo (low-season) yatokanayo
na utalii na bidhaa za kilimo
Kipindi cha mwezi Januari hadi
Aprili ni msimu wa mapato madogo yatokanayo na bidhaa za kilimo na utalii hali
ambayo inachangia upungufu wa dola kwenye soko. Ni matarajio kwamba hali hii
itabadilika katika kipindi cha mwezi Mei hadi Septemba wakati wa msimu wa
utalii na mavuno ya kilimo.
Kuongezeka
kwa malipo ya serikali nje ya nchi (foreign
government obligations)
Malipo ya serikali nje ya nchi yameongezeka katika mwaka
wa fedha 2014/15 yakijumuisha yale ya mashirika ya umma kama TANESCO na TRL.
Chati Na. 5 Malipo ya serikali kwa dola
3. Thamani ya shilingi kwa kipindi cha mwezi April 2015
Katika mwaka ulioshia Machi 2015, shilingi ilishuka
thamani kwa asilimia 13.0. Hata hivyo kwa mwezi April 2015, kasi ya kushuka
thamani iliongezeka ambapo shilingi ilishuka thamani kwa asilimia 8.0 ndani ya mwezi
mmoja tu (Jedwali Na.3).
Jedwali Na. 3: Mwenendo wa thamani ya Shilingi dhidi ya sarafu mbalimbali (badiliko kwa asilimia)
|
Mar-14
to Mar 15
|
31st
Mar-15 to 29th Apr-15
|
US dollar
|
13.0
|
8.0
|
Great Britain Pound
|
1.5
|
12.6
|
Euro
|
-11.7
|
12.0
|
Japanese Yen
|
-4.2
|
9.1
|
Indian Rupee
|
10.1
|
6.7
|
Kenyan shilling
|
6.2
|
5.5
|
Ugandan Shilling
|
-3.2
|
7.8
|
South African Rand
|
0.3
|
11.2
|
Sababu za kushuka thamani kwa kasi:
“Shortage
psychology”na speculation (hisia za
upungufu)
Taharuki iliyoletwa na hisia za upungufu
katika soko zimesababisha ongezeko la mahitaji ya dola hata kwa wale ambao
hawana mahitaji ya kimsingi ya dola. Aidha wengine wanafanya biashara/kamari ya
dola kwa malengo ya kujinufaisha na mabadiliko ya thamani (speculation).
Wasiwasi unaohusiana na uchaguzi (uncertainty)
Katika nchi nyingi ambazo zimekuwa
na historia ya matukio hatarishi wakati wa uchaguzi; wawekezaji na
wafanyabiashara wamekuwa na tabia ya kuhamisha kwa muda mali/fedha zao nje ya
nchi wakisubiri matokeo ya uchaguzi. Katika nchi hizo kumekuwa na tabia ya baadhi
ya watu kuhamisha familia zao kwenda kusubiri matokeo nje ya nchi. Hii imesababisha
ongezeko la mahitaji ya fedha za kigeni ili kukamilisha uhamisho huo. Takwimu
za illicit flows mara nyingi zinaonyesha
kuongezeka kwa kasi ya uhamishaji huo katika kipindi cha uchaguzi. Ingawa kwa
Tanzania, matukio mabaya yanayohusiana na uchaguzi ni nadra, takwimu za illicit
flows zinaonyesha kuwepo kwa uhusiano na election
cycles. Kuna uwezekano mkubwa kuwa sehemu ya taharuki inayohusisha
uhamishaji wa fedha za kigeni imechangia kuongezeka kwa mahitaji.
4. Madhara ya kushuka kwa thamani ya shilingi
i.
Kupanda kwa bei za kuagiza bidhaa
nje (import bill) na hivyo
kusababisha mfumuko wa bei (imported
inflation).
ii.
Kuongezeka kwa mzigo wa malipo ya
mikopo ya nje kwa mikopo ya serikali na ya sekta binafsi.
iii.
Wasiwasi wa uchumi kwenda mrama
unaweza kupunguza uwekezaji.
Wapo Walionufaika:
i.
Wanaouza bidhaa nje wanapata shilingi
nyingi zaidi kwa kila dola. Kwa mfano kwenye biashara ya utalii, wauzaji mazao ya kilimo, bidhaa za viwanda,
madini na kadhalika nje ya nchi.
ii.
Wanaopokea fedha toka kwa jamaa
zao nje (remittances).
iii.
Kuongezeka kwa mapato ya serikali
yatokanayo na kodi za bidhaa na huduma kutoka nje (ushuru wa forodha) pamoja na misaada na mikopo kutoka nje.
5. Matarajio na hatua zinazochukuliwa
Kwa kipindi kijacho mambo makubwa matatu yatasaidia kupunguza kasi ya
kushuka kwa thamani ya shilingi:
i.
Kuanza kwa msimu wa mapato ya
utalii mwezi Mei 2015 ambapo inatarajiwa kuongeza mapato yanayotokana na
shughuli za utalii nchini. Mapato yatokanayo na mauzo ya bidhaa za kilimo nje ya nchi nayo
yanatarajiwa kuongezeka kuanzia mwezi
Agosti 2015.
ii.
Kutolewa kwa fedha za wahisani
(World Bank na AfDB) na kupatikana kwa mikopo yenye masharti ya kibiashara
(ENCB). Matarajio
yetu ni kwamba fedha hizo kutoka nje zitaingia kabla ya mwisho wa mwaka wa
fedha 2014/15. Hali hii itaongeza upatikanaji wa fedha za
kigeni.
iii.
Mategemeo ya kutengemaa kwa uchumi
wa ukanda wa Euro na kuimarika kwa uchumi wa nchi za Ulaya. Hii itaongeza mahitaji
ya bidhaa kutoka Tanzania.
Hatua zinazochukuliwa na Benki
Kuu
Benki Kuu ya Tanzania inaendelea kuchukua hatua mbalimbali, hasa za
utekelezaji wa sera za fedha ili kuimarisha thamani ya shilingi ya Tanzania.
i.
Benki Kuu imeongeza mauzo yake ya
dola kwenye soko la jumla. Katika kipindi cha Januari hadi Aprili 2015, Benki Kuu imeuza dola milioni 339 katika IFEM, takriban sawa na kiasi
kilichouzwa kipindi kama hicho mwaka 2014, ingawa malipo nje ya nchi yalizidi
yale ya mwaka 2014 kwa zaidi ya dola za milioni 300.
ii.
Kupunguza ujazi wa fedha katika
uchumi ili kudhibiti kasi ya ukuaji wa miamala katika soko la fedha za kigeni.
Hii ikiwa ni pamoja na kuongeza SMR ili kupunguza uwezo wa mabenki kutumia
zaidi fedha walizonazo kufanya miamala katika IFEM ili kujinufaisha.
iii.
Kudhibiti biashara za fedha za
kigeni
a.
Swaps: Benki Kuu imeongeza maturity
b.
Net Open Position (NOP)-
Kupunguza kiwango cha fedha za kigeni ambazo mabenki wanaruhusiwa kubaki nazo
ambazo zinaweza kutumika kutafuta faida kwa miamala ya fedha za kigeni.
Matarajio ya mwelekeo wa thamani
ya Shilingi
Kasi ya kushuka kwa thamani ya Shilingi inatarajiwa kupungua katika siku zijazo kutokana na hatua zinazoendelea kuchukuliwa kama ilivyotokea mwaka 2011.
Kasi ya kushuka kwa thamani ya Shilingi inatarajiwa kupungua katika siku zijazo kutokana na hatua zinazoendelea kuchukuliwa kama ilivyotokea mwaka 2011.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni